The House of Favourite Newspapers

FIGA ZA MASTAA MITANDAONI NI FEKI AU HALISI ?

Irene Uwoya

UKIONA mrembo kwenye mitandao ya kijamii ameumbika sana utadhani kachorwa unapaswa kuwa makini, kuna baadhi wanajitengenezea maumbo feki. Kuna program inaitwa Body Builder, katika simu za mikononi. Mastaa mbalimbali Bongo wamekuwa wakiitumia, ‘wame-download’ program hiyo kwenye simu zao ambayo inawawezesha kujitengeneza miili kwa kuweza kujipunguza wanavyotaka au kujiongeza makalio kisha kutuma picha kwenye akaunti zao za mitandao ya kijamii hususan Instagram na kuonekana tofauti.

Mastaa ambao mara nyingi walikumbana na skendo hiyo ya kujipunguza mwili kama tumbo, kiuno na kujiongeza makalio ni Irene Uwoya, Zarinah Hassan ‘Zari’, Aunt Ezekiel na Hamisa Mobeto wakidaiwa kuwa, wanavyoonekana kwenye Instagram na ukiwaona live ni vitu viwili tofauti.

Wakati mwingine hata ukichukua picha zao zilizopo kwenye akaunti au simu za watu wengine, unaweza kukuta ‘kamsambwanda’ hakapo au ‘hips’ zimeyeyuka. Uchunguzi wa mwanahabari wetu umebaini kuwa, wapo baadhi ya mastaa ambao wamekuwa wakifanya michezo hiyo japo wenyewe wamekuwa wakikanusha.

“Mastaa kibao wanafanya hivyo, maumbo unayoyaona kwenye mitandao ya kijamii na ukiwaona live ni vitu viwili tofauti, ukitaka kuamini hili ninalokwambia, watafute mastaa kaa nao karibu uone,” alisema msanii mmoja mkubwa aliyeomba hifadhi ya jina. Gazeti la Amani lilizungumza na baadhi ya mastaa kuhusiana na kutumia program hiyo kwenye simu zao walifunguka kama ifuatavyo:

AUNT EZEKIEL

Muigizaji huyu alisema kuwa anawashangaa sana watu wanaosema kuwa anatumia huo mchezo wa kujitengeneza kitu ambacho hajawahi kukifanya kwa sababu hata akitaka kupungua anafanya ‘diet’ na maisha yanaendelea.

“Sasa mimi nikajitafutie kujiongeza makalio bandia au kujipunguza ili iweje wakati mimi mwenyewe naweza kufanya kwa uhalisia kwanza sifahamu wanafanyaje.”

IRENE UWOYA

Muigizaji huyu yeye alienda mbali zaidi kwa kusema anashangazwa na watu wengi anapoweka picha zake wanasema kajitengeneza huku wamesahau Mungu ana maajabu yake sana kwa mwanadamu. “Hivi mpaka nijitengeneze nafikiria nini, watu wamesahau kabisa Mungu ana maajabu yake sana sasa mimi nitafute uzuri wa kujitengeneza wakati huu hapa wenyewe ni shida hawanijui vizuri tu hao.”

KAJALA MASANJA

Staa huyu ambaye mara nyingi hasumbuliwi na watu wa kwenye mitandao alisema kwanza hajui kabisa jinsi hiyo program inavyotafutwa kwa sababu yeye akiona mwili wake umemzidia anaenda mazoezini kujipunguza lakini siyo kufanya hivyo kwenye simu.

ZUWEMA MOHAMED ‘SHILOLE’

Shilole amesema kuwa anafikiri watu wengi watakuwa ni mashahidi na kumtetea kwa sababu, kipindi hiki kanenepa tu basi kama angetaka kuficha unene wake angetumia board builder lakini anajikubali na jinsi alivyoumbwa.“Basi mimi ningekuwa naifuatilia hiyo kitu ningekuwa nishajipunguza sana maana sasa hivi nimebongeka mno kuliko kitu chochote kile.”

SHAMSA FORD

Kwa upande wake mrembo huyo yeye alisema mara nyingi yupo dukani anawahudumia wateja mbalimbali hivyo akitumia hiyo body builder kujitengeneza hata wateja wake watakuwa hawamuamini hata anachokiuza. “Mimi kwa upande wangu sijawahi kabisa halafu nashindwa kufanya hivyo kwa sababu nipo dukani wakati wote sasa nikiwa najibadili nahisi hata bidhaa zangu watakuwa na wasiwasi nazo.”

Makala: Imelda Mtema

Comments are closed.