The House of Favourite Newspapers

Flora ajiachia na mlinzi wake

mbashaNyota wa nyimbo za Injili Bongo, Flora Mbasha (kushoto) akiwa katika pozi na kijana anayedaiwa kuwa mlinzi wake, Peter.

Brighton Masalu
GUMZO! Miezi kadhaa imekatika tangu nyota wa nyimbo za Injili Bongo, Flora Mbasha kumwagana na mumewe, Emmanuel Mbasha ‘Imma’, habari ya mjini kwa sasa ni mwanadada huyo kudaiwa kujiachia kila kona na jamaa anayemtambulisha kwa jina moja la Peter akisema kuwa ni mlinzi wake wa karibu, Risasi Jumamosi linatumbua jipu!

TUJIUNGE NA CHANZO
Kwa mujibu wa chanzo makini, wawili hao wamekuwa wakionekana katika hafla mbalimbali wakitembea kama kumbikumbi hali ambayo imekuwa ikizua minong’ono kuwa huenda jamaa huyo ni m’badala wa Emmanuel.
“Hivi hamna habari? Yaani tangu Flora amwagane na Mbasha, amekuwa akiongozana na Peter kila mahali, eti ndiye mtu wake wa karibu. Wamekuwa wakionekana hoteli pamoja, mara katika hafla mbalimbali. Yaani sasa hivi siyo siri, kila mtu anajua ni mtu na mwenzake,” kilisema chanzo hicho.

mbasha2Flora Mbasha.

CHANZO CHAANIKA PICHA
Kuonesha kuwa hakibahatishi, chanzo hicho kilimtumia picha mwandishi wetu inayomuonesha Peter na Flora wakiwa katika pozi la kugusanisha vichwa vyao nyuma kukiwa na tanki la maji.
“Kama vipi ngoja nikutumie picha hii ujionee mwenyewe maana nikisema hawa watu wapo karibu sana namaanisha ukaribu haswaa,” kilisema chanzo hicho huku kikimtumia picha mwandishi wetu.

ema-mbashaEmmanuel Mbasha ‘Imma’

UKARIBU WAO ULIANZA ZAMANI!
Baada ya mwandishi wetu kutumiwa picha hiyo, ‘kiranja’ wa gazeti hili alivuta kumbukumbu katika makabrasha yake na kubaini kuwa, wawili hao walianza kuwa karibu kwa muda mrefu lakini ukaribu wao ulikolea zaidi wakati wa kesi ya Imma akidaiwa kumbaka shemejiye iliyokuwa ikiunguruma kwenye Mahakama ya Wilaya ya Ilala, Dar.

RISASI LILIWAHI KUWAKUTA PAMOJA!
Kumbukumbu zilionesha kuwa, siku moja kwenye viunga vya mahakama hiyo Peter na Flora walionekana wakiwa ‘klozdi’ na katika utambulisho alioufanya Flora kwa mwanahabari wetu alisema jamaa huyo ni mtu anayemtumia kama mlinzi wake wa karibu.

PETER KIZIMBANI
Ili kujua tofauti ya tui na maziwa, mwanahabari wetu alimtafuta Peter kwa njia ya simu na kumsomea madai hayo ambapo alijitetea kuwa, yeye na mwimba Injili huyo si wapenzi ila ni ndugu.
“Aah! Kaka, hakuna bwana! Unajua hizo ni mbinu za Imma (Mbasha) kutaka kutuchafua mimi na Flora. Mimi ni ndugu yake Flora, nadhani hata siku ile pale mahakamani Ilala ulitambulishwa hivyo,” alisema Peter.

FLORA AIBUKA MZIMAMZIMA!
Dakika kadhaa baada ya mwandishi wetu kuzungumza na Peter juu ya jambo hilo, mara simu yake ya mkononi iliita na alipoangalia jina la mpigaji alikuwa Flora, haraka sana simu ikapelekwa sikioni kutaka kusikia shida yake:
“Kaka, nasikia umempigia simu Peter na kumuuliza kuhusu ukaribu wangu na yeye. Kwanza samahani kama amekujibu vibaya. Unajua yeye huwa si mtu wa kuzungumza sana na ana hasira za karibu.
“Lakini ukweli ni kwamba, yule ni ndugu yangu, japokuwa ni kweli niko naye karibu. Wakati mwingine namtumia kama mlinzi wangu. Si unajua wakati niko kwenye mfarakano na Imma, kulikuwa na vitisho vingi, hivyo familia yangu ilimteua yeye kuwa mlinzi wangu, ndiyo maana kila nilipo lazima na yeye awepo, maana nikipatwa na lolote wa kwanza kuulizwa atakuwa yeye.
“Hakuna kingine zaidi ya hapo lakini naomba hayo mambo uachane nayo, yatazua mjadala mwingine usiokuwa na maana.”

IMMA ANAMJUA PETER?
Ili kuzidi kuishibisha habari hiyo, Risasi Jumamosi lilimtafuta aliyekuwa mume wa Flora, mista Mbasha mwenyewe ili kujua kama anafahamu chochote kuhusiana na ukaribu wa Peter na mkewe waliyetengana.
“Hata mimi nasikiasikia tu hizo habari lakini kimsingi sihitaji sana kuzitilia maanani maana mimi kwa sasa naangalia maisha yangu, yaliyotokea yameshatokea na nimemwachia Mungu.
“Ukaribu wao uwe wa kawaida, usiwe wa kawaida, mimi sijali. Nimeshaacha kabisa kumfuatilia huyo mtu (Flora),” alisema Mbasha.

KUMBUKUMBU
Flora na Mbasha ndani ya ndoa yao iliyoparaganyika mwaka jana, walifanikiwa kupata mtoto mmoja aitwaye Elizabeth ‘Liz’, waliachana baada ya Mbasha kutuhumiwa kumbaka shemeji yake huyo kisha kesi kuunguruma mahakamani ambapo hukumu ilipotolewa Septemba mwaka huu, Mbasha hakupatikana na hatia.

Comments are closed.