The House of Favourite Newspapers

Genevieve: Miss Tanzania 2010 Anayevaa Viatu Vya K-Lyinn

0
Miss Tanzania 2010, Genevieve Emmanuel.

NA ANDREW CARLOS | GAZETI LA IJUMAA | SHOWBIZ

UKIAMBIWA utaje ma-miss walioteka katika Muziki wa Bongo Fleva moja kwa moja utamtaja Mwanamuziki, Jacqueline Ntuyabaliwe ama wengi wamezoea kumuita K-Lyinn.

K-Lyinn alikuwa mmoja wa wanamuziki warembo wa kike aliyesumbua kwenye muziki huo na ngoma kibao kama Nipe Mkono aliomshirikisha Mr Blue, Nikipata Wangu akiwa na Jay Moe, Chochote Utapata akiwa na Noorah pamoja na Crazy Over You aliomshirikisha Squeezer.

Mrembo wa taji la Miss Tanzania 2000, Bi. Jacqueline Mengi akizungumza jambo.

Licha ya kulikamata soko la muziki akiwa kama Miss Tanzania 2000 pekee katika kipindi chake hicho, K-Lyinn alifanikiwa kuibuka na albamu moja iliyotambulika kama Nalia kwa Furaha ambapo ngoma hiyo iliyobeba jina la albamu alishirikiana na Bushoke.

Genevieve Emmanuel akiwa kwenye pozi.

Licha ya kujizolea mashabiki wengi, baada ya miaka kadhaa mbele, K-Lyinn aliamua kupumzika kufanya muziki ambapo tangu kipindi hicho hakutokea tena mshiriki ama mshindi wa Miss Tanzania kufanya muziki.

Lakini kwa hivi karibuni wapo walimbwende kadhaa ambao wamejitosa kuziba pengo la K-Lyinn katika kufanya Muziki wa Bongo Fleva na wameanza kukubalika, miongoni mwa walimbwende hao ni Miss Pwani 2013 (Lulu Abbas ‘Lulu Diva’) pamoja na Miss Tanzania 2010, Genevieve Emmanuel.

Kwa upande wa Lulu Diva anafanya poa sokoni akiwa na ngoma mbili, Malele na Usimwache wakati Genevieve anabamba na Ngoma ya Nana iliyopikwa na Prodyuza Luffa huku kioo kikisimamiwa na Dairekta Ivan.

Showbiz ilipata nafasi ya kukutana na Genevieve ambapo alifungukia mambo yake mengi ya muziki na maisha na katika makala haya anafunguka zaidi;

Showbiz: Nani alikushawishi kuingia katika muziki?

Genevieve: Muziki ni kipaji changu na ni moja ya kitu nilichokuwa nikikipenda sana. Ni watu tofauti waliokuwa wakinihamasisha na kuniambia muziki utanifanya niwe huru na kuniletea mafanikio.

Showbiz: Una ngoma ngapi hadi sasa?

Genevieve: Ninazo nyingi tu
ambazo nimeshazirekodi lakini kwa majina yake siwezi kutaja kwa sasa hadi pale nitakapotaka kuziachia.

Showbiz: Changamoto zipi unapitia katika muziki wako?

Genevieve: Changamoto kubwa ni kufanya vizuri sokoni. Nashukuru video na Wimbo wa Nana unafanya vizuri.

Showbiz: Muziki unaofanya nani anahusika kutunga mashairi?

Genevieve: Sina mtu maalum anayenitungia ila mara nyingi huwa nafanya kama kuchukua mawazo kutoka kwa watu ninaokutana nao kama Maprodyuza (Luffa) ambao wananisaidia katika kutunga. So prodyuza yeyote ninayemkuta studio ninayotaka kutengeneza nyimbo huwa nashirikiana naye katika mawazo.

Showbiz: Nani alihusika katika ‘idea’ ya Video ya Nana?

Genevieve: Idea nzima ilikuwa ni ya Dairekta (Ivan), alitupa taswira ambayo anataka kutengeneza katika video yangu so nikatafuta modo pamoja na eneo la tukio tukafanya.

Showbiz: Una menejimenti?

Genevieve: Nipo chini ya menejimenti ya Hexagon Entertainment ndiyo wanaonisimamia mambo yote yanayohusiana na muziki, mimi ni msanii wa kwanza kwao kunisimamia.

Showbiz: Malengo yako yapoje katika muziki?

Genevieve: Kwanza ni kufanya muziki mzuri na kuachia nyimbo ambazo zitaweza kuishi kwa muda mrefu, kuleta uhalisia pia kukonga nyoyo za mashabiki wangu.

Mara nyingi huwa naamini katika kufanya kitu kizuri ambacho kitadumu na naamini nitavaa viatu vya K-Lyinn. Showbiz: Tangu umeachana na u-miss ni kitu gani ulikuwa ukikifanya?

Genevieve: Siwezi kusema kuwa nimeachana kabisa na masuala ya ulimbwende au u-miss lakini nimebakia kuwa kama mdau na kushirikiana na Kamati ya Miss Tanzania katika masuala tofauti, ‘other than that’ nilikuwa nikiendelea tu na maisha yangu, kufanya biashara na vinginevyo. Mimi ni mtu ‘private’ na huwa napenda nijulikane ‘specifically’ kwa jambo ninalofanya.

Showbiz: Una mchumba, mtoto? Na mchumba wako anachukuliaje muziki unaofanya?

Genevieve: Hapana sina mtoto wala mwanaume kwa sasa. Muziki wangu ninaofanya nasapotiwa asilimia 100 na familia na marafiki zangu wa karibu.

Showbiz: Mastaa gani nchini unatamani kufanya nao kazi?

Genevieve: Napenda kufanya na mastaa wengi tu.

Ningependa hasa kushirikiana na wakongwe ili pia iwe fursa ya kujifunza zaidi. So sibagui, sichagui! Swali ni je, mwanadada huyu atafanikiwa kuvaa viatu vya K-Lyinn? Tusubiri tuone

Leave A Reply