Gereza la Guantanamo liko Cuba si Marekani!
JE, unaufahamu wimbo wa Guantanamera? Ni moja ya nyimbo maarufu zaidi katika kumbi za muziki duniani! Kwa kifupi, Guantanamera ni mwanamke kutoka Guantanámo. Kwa lugha za asili ya Kilatini kama Kihispania ambayo ndiyo lugha ya Cuba, Guantanámo ni neno la jinsia ya kiume (masculine), ambapo jinsia ya kike (feminine) ni Guantanamera!
Kwa hivyo, unavyosikia wimbo wa Guantanamera katika kumbi za Magomeni (Dar), Mwanjelwa (Mbeya) na Kashai (Bukoba) ujue mwimbaji ‘anamlilia’ au anambembeleza mwanamke kutoka Guantanámo.
Kwa waliowahi kufika Cuba, Guantanámo ni ghuba iliyo katika jimbo (mkoa) wa kusini-mashariki mwa kisiwa maarufu cha Cuba ambako Marekani iliamua kuwafunga inayowaita magaidi dhidi yake – kutoka Afghanistan, Iraq na kwingineko duniani – katika Gereza la Guantanámo.
Kwa kifupi, Marekani ililichukua eneo la Guantanáno kwa ‘maguvu’ mwaka 1903 kwa mkataba wa miaka 99, baada ya nchi hiyo kushinda vita dhidi ya Hispania iliyokuwa inaitawala Cuba. Tangu wakati huo, Marekani imekuwa ikilitumia eneo hilo kama kituo cha kijeshi na sasa imelifanya kuwa gereza pia.
Hata hivyo, baada ya utawala wa Kikomunist wa Fidel Castro, kuingia madarakani, Cuba imekataa tangu mwaka 1959 kupokea hata senti moja ambayo ni malipo ya mkataba huo ikiitaka Marekani iondoke Guantanámo. Marekani nayo imekuwa ikitumia ubabe wa kutoondoka eneo hilo.
Guantanámo ni ghuba na mji ulio mashariki mwa Cuba ukiwa na wakazi wapatao 244,000 ukijulikana kwa Kihispania kama Bahía de Guantánamo ikiwa imezungukwa na milima ‘iliyoitenga’ na eneo jingine la Cuba.
Wanasiasa wa Marekani walioamua kuwafunga ‘magaidi’ waliowakamata na kuwapeleka Guantanámo – enzi ya utawala wa George Bush na viongozi waliofuata – walifanya hivyo kwa kujua kwamba iwapo pangetokea zahama ya gereza hilo la Guatanámo kuvamiwa na kushambuliwa, nchi ambayo ingepata madhara kwanza ni Cuba, si Marekani.
Kisiwa cha Cuba kiko umbali mrefu wa zaidi ya kilomita 1,000 kutoka Marekani.