The House of Favourite Newspapers

GLAUCOMA; UGONJWA USIO NA DALILI UNAOSABABISHA UPOFU

 GLAUCOMA ni ugonjwa hatari sana na tata ambao huathiri seli za macho zinazosaidia kuona na huweza kusababisha mtu kupoteza uwezo wa kuona.  Ni ugonjwa unaochangiwa na mgandamizo mkubwa ndani ya macho unaosababishwa na majimaji yanayoingia na kutoka kwenye jicho. Ugonjwa wa Glaucoma ni tofauti na Trakoma. Trakoma husababishwa na bakteria aina ya Chlamydia Trachomatis. Kwa kawaida husambazwa na inzi kuanzia kwa mtu mmoja hadi mwingine.

Kutokana na asili ya ugonjwa huo, umesababisha ujulikane kama mwizi wa macho anayekuja kwa kunyatia. Hii inatokana na ugonjwa huo kutokuwa na dalili, unakuja taratibu sana na ghafla mtu hupoteza uwezo wa kuona na kupata upofu wa kudumu.

Ugonjwa wa Glaucoma unaripotiwa kuwa moja ya sababu zinazoongoza katika kusababisha upofu duniani. Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO), watu milioni 4.5 duniani wamekuwa vipofu kutokana na ugonjwa huo.

Shirika la Utafiti wa Glaucoma (GRF) linasema zaidi ya asilimia 40 ya uwezo wa kuona unaweza kupotea bila mtu kujua. Glaucoma ni ugonjwa wa pili na unaoongoza kwa kusababisha upofu duniani kote. Katika kila watu 100, zaidi ya watano wanakadiriwa kuwa na aina hii ya ugonjwa.

Glaucoma siyo jina la ugonjwa wa jicho pekee, bali linahusu kundi la ugonjwa wa macho ambao unakusababishia upofu taratibu siku hadi siku bila dalili yoyote.

Upofu huo unasababishwa na kuharibika kwa neva za macho. Neva hizi zipo kama kebo za umeme wenye nyaya zaidi ya milioni na ndiyo ina kazi ya kupeleka taswira kwenye ubongo. Shinikizo kwenye jicho ndiyo chanzo cha uharibifu wa neva hizi. Endapo neva za macho zikiharibiwa, mtu hupoteza uwezo wa kuona na kamwe hawezi kupona. Kuna aina mbalimbali za Glaucoma, ikiwa ni pamoja na Primary Open Angle Glaucoma ambayo ni Glaucoma ya kawaida duniani kote.

Kwa namna inavyotokea mirija ya maji pembeni ya macho inachoka kadiri muda unavyokwenda na shinikizo ndani ya macho huongezeka hatua kwa hatua. Aina ya pili ni Primary Angle Closure Glaucoma aina hii inafahamika sana. Mirija inakosa uwezo wa kutoa majimaji nje ya jicho na hivyo kusababisha mgandamizo ndani ya jicho.

Aina nyingine ni ile ya kuzaliwa ambayo hutokea mara moja katika watoto 1,000 wanaozaliwa na inaweza kusababisha upofu takriban kwa asilimia 10 ya matukio. Glaucoma ya kuzaliwa nayo inatokana na matatizo ya mfumo. Hali hiyo inatokana na macho ya watoto wachanga kuongezeka na yanakuwa na rangi nyeupe.

TIBA NA USHAURI

Vitu kama majeraha kwa jicho au baadhi ya dawa zinaweza kuzuia kutoka kwa majimaji na kuchangia kusababisha Glaucoma. Pia wagonjwa wa pumu, mzio wa ngozi na macho, mara nyingi hutumia dawa ambazo zina steroidi ambayo inaweza kusababisha Glaucoma.

Ugonjwa huo kwa kawaida huiba uwezo wa kuona kimyakimya. Mara nyingi Glaucoma haiwezi kutibiwa. Matibabu yake hutolewa ili kuhifadhi uwezo mdogo wa kuona uliobakia. Ni vizuri kufanya uchunguzi wa kina wa Glaucoma kabla ya mpango wowote wa matibabu. Natoa wito kwa Watanzania kujijengea utamaduni wa kufanya uchunguzi wa macho mara kwa mara ili kuchukua tahadhari.

Comments are closed.