The House of Favourite Newspapers

GLOBAL WALIVYOTOA SHUKRANI KWA MAVENDA, WASOMAJI WAKE

Meneja wa Global Publishers, Abdallah Mrisho akijibu maswali yaliouliza na mavenda (hawapo pichani) pembeni yake Eric Shigongo akimsikiliza.

JUMAPILI ya juzi, Julai 15 ilikuwa ni siku ya burudani mwanzo mwisho kwa wakazi wa Jiji la Dar wa Salaam na mikoa ya jirani kufuatia shoo bab’ kubwa iliyoporomoshwa na wasanii wakali Bongo, Roma, Juma Nature na Man Fongo.

Shoo hiyo ya bure kabisa iliyoporomoshwa kwenye tamasha lililopewa jina la Tusua Maisha na Global lililoandaliwa na Kampuni ya Globa Publishers kwa lengo la kuwashukuru wasomaji na wauzaji wa magazeti, wachapishaji wa Magazeti ya Risasi, Championi, Uwazi, Ijumaa, Amani, Ijumaa Wikienda na Spoti Xtra, ilichukua nafasi ndani ya Ukumbi wa Dar Live, Mbagala Zakhem kuanzia mchana hadi kigiza kinaingia na kukutanisha waandaaji, wasomaji na wauzaji wa magazeti hayo.

Mkurugenzi wa Global Publishers, Eric Shigongo akizungumza na mavenda (hawapo pichani).

Mbali na wadau hao kukutana kisha kupiga msosi pamoja na kubadilishana mawazo juu ya biashara ya magazeti na promosheni ya Tusua Maisha na Global, nafasi ilipatikana kwa wao kushuhudia burudani za kukata na shoka.

MAN FONGO KWELI NOMA

Mkali wa singeli Bongo, Man Fongo ndiye aliyeanza kupagawisha maelfu ya watu waliotinga katika viwanja hivyo kwa kuimba nyimbo zake kama vile Kujinafasi, Sio Poa na kionjo cha Hainaga Ushemeji, hali iliyosababisha nderemo na vifijo vitawale eneo hilo.

NATURE AKAMUA, ATOA ZAWADI

Juma Nature kama kawaida yake alidhihirisha kuwa bado muziki wake unatamba kwani baada ya kupanda jukwaani akiwa ameongozana na KR Mulla, alikamua nyimbo zake kali zikiwemo Kigetogeto, Sonia na kuwafanya watu wapagawe ile mbaya. Katikati ya shoo, Nature alisema kuwa jasiri haachi asili na kazi yake ni kutoa burudani na kuwataka mashabiki kuwa na upendo na kuendelea kusoma Magazeti ya Global.

Aidha katika tamasha hilo, Nature alipewa jukumu la kukabidhi zawadi ya pikipiki kwa Amiri Bakari wa Ubungo na Solomoni Mapunda wa Mbagala baada ya wasomaji hao kuibuka washindi katika shindano linaloendeshwa na Global linalokwenda kwa jina la Tusua Maisha na Global.

ROMA AZUIA WATU KOMBE LA DUNIA

Naye Msanii wa Hip Hop, Roma ambaye alipanda jukwaani baada ya Nature, alijikuta akiwazuia watu kibao kuangalia mechi ya Fainali za Kombe la Dunia kati ya Croatia na Ufaransa kufuatia shoo yake kali aliyokuwa akiporomosha.

Roma kama kawaida yake alikiteka kijiji na kuimba nacho nyimbo zake kibao zikiwemo Mathematics, Zimbabwe na nyinginezo, jambo ambalo liliwafanya hata wale waliokuwa wakiangalia mechi hiyo kwenye ‘screen’ kubwa iliyopo uwanjani hapo kuipa kisogo na kugeukia shoo ya msanii huyo.

WASOMAJI WAISHUKURU GLOBAL

Kutokana na kile walichoandaliwa siku hiyo, wasomaji mbalimbali wa magazeti ya Global walitoa shukurani zao na kuahidi kuendelea kununua bidhaa za kampuni hiy

“Kwa kweli nimefarijika sana, Global wameonesha kutujali sana, nilikuwa sijawahi kuingia kwenye ukumbi huu lakini leo nimeingia na kupata burudani. Pia nimepata bahati ya kukutana na waandishi wengi ambao nilikuwa nasoma tu kazi zao, pilau pia tumekula, nimefurahi sana kwa kweli,” alisema msomaji huyo aliyejitambulisha kwa jina la Alfred Warren. Naye mmoja wa wauzaji wa magazeti ya Global anayefanya kazi zake maeneo ya Kariakoo jijini Dar alisema: “Imekuwa ni siku ya kipekee sana kwetu wauzaji wa magazeti, tumeburudika na kunufaika kwa mengi, kilichobaki sasa ni kuunga mkono jitihada za Global katika jukumu lao la kuhabarisha, kuelimisha na kukosoa. Tutahakikisha tunauza magazeti na kuwafikia watu wengi.”

NENO KUTOKA GLOBAL

Mkurugenzi wa Global Publishers, Eric Shigongo aliwashukuru wote waliojitokeza katika tamasha hilo na kuwaeleza kuwa, wana mchango mkubwa katika kukua kwa kampuni hiyo tangu ilipoanza mwaka 1998. “Nawashukuru wote kwa kuacha kazi zenu na familia, mmekuwa muhimu sana kwani bila mavenda na wasomaji Global isingekuwepo. Tumekuja hapa kuwasikia, mseme kila kitu tutafanyia kazi.

“Kuna wengine wameleta maoni yao ya tisheti na kofia, zawadi kila wiki kwa mavenda watakaofanya vizuri hilo tutalifanyia kazi haraka iwezekavyo kuanzia wiki ijayo. Tumeshirikiana nanyi kwa muda mrefu, tulishawahi kutoa shilingi milioni 7 katika Saccos yenu, kiufupi uhusiano wetu umekuwa mzuri,” alisema Shigongo.

Comments are closed.