Global yampa tuzo za heshima Samatta (Picha +Video)

MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Tanzania na nahodha wa timu ya Taifa, Taifa Stars, Mbwana Samatta jana alitunukiwa tuzo mbili za heshima na uongozi wa Global Group kupitia magazeti yake ya michezo ya Championi na Spoti Xtra kutokana na kuiwakilisha vema Tanzania kimataifa.

Samatta anayecheza soka la kulipwa katika klabu ya KRC Genk inayoshiriki Ligi Kuu Ubelgiji ametunukiwa tuzo hizo kutokana na mafanikio makubwa aliyopata katika msimu uliopita baada ya kuipa ubingwa timu yake pamoja na kufunga mabao 23 akiwa nyuma ya mfungaji bora.

Tuzo hizo zilitolewa jana katika ofisi za Global Group zilizo Sinza Mori jijini Dar baada ya kufanya ziara maalum ya kutembelea na kujionea shughuli mbalimbali zinazofanywa na kampuni hiyo. Samatta alipewa tuzo ya kiatu cha dhahabu ambayo alikabidhiwa na Mhariri Mtendaji wa Global Publisher, Saleh Ally ‘Jembe’ iliyokuwa na ujumbe ‘Mguu wa dhahabu 2019 Mbwana

Samatta’ ikiwa inalenga kuthamini mchango wake mkubwa kutokana na rekodi za mabao alizofanikiwa kuweka kwenye sehemu zote alizopita. Wakati tuzo ya pili aliyopewa ilikuwa ikisomeka tuzo ya mfano wa kuigwa Mbwana Samatta 2019 kutokana na mafanikio makubwa aliyopata katika timu zote alizopita ikiwemo kucheza kombe la dunia ngazi ya klabu, kushinda tuzo ya mchezaji bora wa Afrika wanaocheza ligi ya ndani kwani imekuwa chachu kubwa ya wengi kufuata nyayo zake.

Saleh alisema: “Tuzo hii tumempa kwa sababu amekuwa mfungaji bora karibu kila sehemu aliyokwenda pamoja na ugumu wote aliokutatana nao, ameonyesha uwezo mkubwa wa kufunga kwa sababu katika klabu zote alizopita.
“Lakini hii nyengine inasema mfano wa kuigwa Mbwana Samatta 2019, mnajua tangu amekwenda DR Congo amechukua makombe mengi, amecheza kombe la dunia ngazi ya klabu nafikiri yeye na Thomas Ulimwengu kwa Tanzania, amekuwa mchezaji bora wa Afrika kwa wanaocheza ligi ya ndani na mfano wa kuigwa kutokana kuhamasisha watu kujituma,” alisema Ally.

PICHA NA RICHARD BUKOS | GPL


Comments are closed.