The House of Favourite Newspapers

Gomes: Waleteni Tu Hao Yanga SC

0

KOCHA Mkuu wa Simba, Mfaransa, Didier Gomes, amesema kuwa michezo mitatu ya Kanda ya Ziwa aliyoicheza na kupata kuvuna pointi tisa, imempa kiburi na kutamka kuwa kikosi chake kimeiva na kipo tayari kucheza na timu yoyote, ikiwemo Yanga.

 

Kauli hiyo aliitoa mara baada ya kufanikiwa kupata ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Gwambina FC juzi Jumamosi kwenye Uwanja wa Gwambina Complex, Misungwi, Mwanza.

 

Simba na Yanga zinatarajiwa kuvaana Mei 8, mwaka huu kwenye Uwanja wa Mkapa jijini Dar es Salaam katika mchezo wa Ligi Kuu Bara. Katika mzunguko wa kwanza, timu hizo zilitoka sare ya 1-1.

Akizungumza na Championi Jumatatu, Gomes alisema kuwa anafurahishwa na mwenendo wa kikosi chake kuelekea mchezo huo mkubwa wa Ligi Kuu Bara dhidi ya Yanga Gomes alisema kuwa michezo ya Kanda ya Ziwa aliitumia vema kukijenga zaidi kikosi chake kwa kufanyia marekebisho baadhi ya sehemu zilizokuwa zina upungufu ili kuhakikisha makosa hayo hayajitokezi watakapovaana na Yanga.

 

Aliongeza kuwa pia amepanga kukijenga zaidi kikosi chake katika mchezo ujao wa ligi watakapocheza na Dodoma Jiji kabla ya kukutana na Yanga.

 

“Tumeshinda michezo yetu miwili ugenini sio jambo rahisi lakini wachezaji wangu wamekuwa wakipambana ili kuhakikisha tunatimiza malengo yetu ya kupanda kileleni mwa msimamo.“Lengo letu ni ubingwa wa ligi utakaotuhakikishia kucheza michuano ya kimataifa katika msimu ujao, hivyo nimeitumia vema michezo hii ya Kanda ya Ziwa kwa kuboresha kikosi changu,” alisema Gomes

STORI: WILBERT MOLANDI, Dar es Salaam

Leave A Reply