The House of Favourite Newspapers

The Graves of The Innocents (Makaburi ya Wasio na Hatia)- 39

0

ILIPOISHIA:

Nilifungua zipu kisha nikaanza kufanya kama vile nilivyoelekezwa. Nikiwa naendelea na kitendo kile cha aibu na cha aina yake, nilisikia watu wote waliokuwa sebuleni wakishtuka, nadhani waliniona nilichokuwa nakifanya, sikuwajali, nikaendelea kuumwaga, mara kilisikika kishindo kikubwa ambacho kilinifanya nishindwe kuendelea kufumba macho, nikayafumbua.

“Mungu wangu!” nilisema kwa sauti ya juu.

SASA ENDELEA…

Kile kilichokuwa kikinitoka, hakikuwa haja ndogo kama mwenyewe nilivyokuwa nadhani, ilikuwa ni damu, tena nzito kabisa yenye wekundu uliokolea kisawasawa, na kile kishindo kilichosikika, kilikuwa ni cha dude kubwa lililoanguka kutoka angani.

Sijui niliiteje dude hilo kwa sababu kwanza lilikuwa na miiba kama nungunungu, lakini pia lilikuwa na mabawa yenye kucha kama popo, ukubwa wake ulikuwa kama ng’ombe mdogo.

Usoni lilikuwa na pembe zilizojikunja na sehemu ya macho, kulikuwa kumezibwa kabisa, kwa kifupi halikuwa na macho. Ile damu iliendelea kunitoka, hata pale nilipotaka kuikata haja ndogo, iliendelea kunitoka kwa wingi utafikiri inavutwa na bomba.

Lile dude la ajabu, lilijiburuta chini na kusogea mpaka pale nilipokuwa natolea haja ndogo, kwenye vizingiti vya milango, likafumbua mdomo kidogo na kutoa ulimi mrefu uliokuwa umegawanyika katikati kama wa nyoka, likaanza kulamba kile nilichokuwa nakitoa.

Naomba nieleze vizuri kilichotokea na ambacho huwa kinatokea pale mtu anapokumbwa na nguvu za uchawi. Yaani tukio unaliona, na ile hatari iliyopo mbele yako unaiona kabisa lakini mwili unakufa ganzi, unakuwa huwezi kufanya chochote zaidi ya kile ambacho unakuwa umeshaanza kukifanya na akili zako zinakosa maamuzi, kwa kifupi unakuwa siyo wewe.

>>Usiache kutembelea Simulizi za Majonzi

Hicho ndicho kilichotokea, sikuwa na uwezo wa kuikatisha ile haja ndogo ya damu, sikuwa na uwezo wa kwenda mbele, wala sikuwa na uwezo wa kurudi nyuma, nilitamani kupiga kelele za kuomba msaada lakini pia sikuweza kufanya hivyo, nikabaki nimeduwaa tu.

Lile dude lililamba ile damu yote pale mlangoni, likaona haitoshi, likafumbua mdomo wake ambao ulikuwa na meno mengi na kukinga ile iliyokuwa ikiendelea kunitoka kupitia haja ndogo, nikasikia kitu kama ganzi ikinipata kwenye maeneo yangu nyeti kisha ile damu ikakata.

Lile dude ambalo ama kwa hakika lilikuwa linatisha, likajilamba na kugeuka, likajikung’uta kwa nguvu kwenye mabawa yake yenye kucha kubwa na kali, likawa kama linataka kuruka kwani lilipigapiga mbawa zake, kufumba na kufumbua, likayeyuka na kupotea.

Lilipopotea tu, nilihisi kichwa kikiwa kizito, nikaanza kuona giza machoni mwangu, nikawa nasikia sauti za ajabuajabu masikioni, nikadondoka chini kama mzigo. Sikuelewa tena kilichoendelea.

***

Nilipokuja kuzinduka, nilijikuta nimelala chini kwenye majani, mwili wangu ukiwa unahisi baridi kali kuliko kawaida. Kilichonizindua zilikuwa ni kelele za ngoma na manyanga na sauti za ajabuajabu za watu wakiimba nyimbo kwa lugha ambayo sikuwa naielewa.

Nilifumbua macho, huku mapigo yangu ya moyo yakiwa yananienda mbio kuliko kawaida, macho yangu yalitazama juu moja kwa moja. Nikawa naziona nyotanyota kwa mbali kuashiria kwamba ni usiku sana, lakini pia upande wangu wa kushoto, kulikuwa kumewashwa moto mkubwa ambao ulipafanya pale nilipolala, pawe na mwanga.

Niligeuza shingo kutazama pale ni wapi, nilishtuka kugundua kwamba kumbe nilikuwa katikati ya duara, watu wengi waliokuwa hawana kitu mwilini zaidi ya kujiziba kidogo na nguo nyeusi au nyekundu kwenye maeneo nyeti walikuwa wamenizunguka. Wengine ambao ni wanawake, walikuwa wamejiziba pia vifuani mwao.

>>Usiache kutembelea Simulizi za Majonzi

Walikuwa wakiimba na kucheza kwa kuzunguka duara ambalo ndani yake nilikuwa nimelazwa mimi na pia kulikuwa na moto mkubwa jirani kidogo na pale nilipokuwa nimelala. Walikuwa wakiimba na kucheza, huku kila mmoja akionesha kuwa na furaha kubwa.

Nilishtuka mno, nikawa sielewi pale ni wapi na nimefikaje, nilijaribu kuwatazama watu hao kwenye nyuso zao kama kuna yeyote ninayeweza kumtambua lakini macho yangu hayakuwa na nguvu za kutosha kuona. Nilitaka kusimama lakini nilishtuka zaidi kugundua kwamba kumbe nilikuwa nimefungwa mikono na miguu kwa kamba za miti.

Zile purukushani zangu, ziliwafanya wale watu waache kila walichokuwa wanakifanya, wote wakawa wananitazama. Niligeuka huku na kule, wote walikuwa wamenikazia macho. Kilichozidi kunitisha, macho yao yalikuwa yakiwaka kama wanyama wakali wa porini.

Nikamsikia mmoja kati yao akizungumza kwa lugha ambayo sikuwa naielewa, watu wote wakainua mikono juu kisha taratibu wakaishusha chini, wakati wakishusha mikono, nao walishuka mpaka wakapiga magoti, wakapeleka vichwa vyao mpaka chini kisha wakainuka na kusimama kama mwanzo.

Yule mwanaume ambaye sikuwa najua yupo upande gani, aliyarudia tena maneno yale, wakafanya hivyo tena mpaka chini, wakarudia mara tatu kisha wote wakakaa chini na kukunja miguu.

Kizee kimoja kilichokuwa kimepinda mgongo, kiliibuka kutoka kusikojulikana, kikiwa kinatembelea mkongojo. Kikawa kinajikongoja kuja pale nilipokuwa nimefungwa, kadiri kilivyokuwa kinanikaribia ndivyo mapigo ya moyo wangu yalivyokuwa yakizidi kuongezeka.

Sikujua kinataka kunifanya nini, kilisogea mpaka pale nilipokuwa nimefungwa, nikakiona kikitoa kisu kikali, kikaniinamia huku kikiyumbayumba, nikajua nimekwisha. Nimewahi kusikia kwamba wachawi wana mchezo wa kuchinja watu na kuwala nyama, nikajua na mimi ndiyo siku yangu ya kuliwa imewadia.

Tofauti na nilivyotegemea, wala hakunidhuru mwilini, badala yake alikitumia kile kisu kukata kamba nilizofungwa mikononi na miguuni. Kilichonishangaza zaidi, kumbe alikuwa akinijua mpaka jina langu kamili.

“Togolai!”

“Naam, shikamoo babu,” niliitikia kwa kutetemeka. Hakujibu salamu yangu, badala yake alinionesha sehemu ya kukaa, akaniambia kwa ishara nikunje miguu kama watu wengine wote walivyokuwa wamekaa. Nilitii agizo hilo haraka.

Kumbe pembeni ya pale nilipokuwa nimelazwa, kulikuwa na vifaa mbalimbali, nikamuona akichukua kibuyu kimoja, akakitingisha kisha akanipa na kunionesha kwa ishara kwamba ninywe kilichomo ndani.

Huku nikitetemeka, nilikishika kibuyu hicho, nikawa nakipeleka mdomoni huku nikimtazama kwa kina mzee huyo, pamoja na watu wengine waliokuwa wamenizunguka kwa mbali.

“Nwa, ulogoleza shoni, nwa!” aliongea kwa kilugha ambacho sikuwa nakielewa lakini kwa jinsi matamshi yake yalivyokuwa, nilihisi ananiambia, ‘kunywa, unaogopa nini, kunywa’.

Nilipokisogeza kibuyu hicho karibu na pua, nilikumbana na harufu kali kwelikweli, ikabidi nizibe pua, nikanywa huku nikiwa nimefumba macho. Kabla sijameza, nilisikia vitu vikinitembea mdomoni, nilipotazama vizuri kile kibuyu, pale kwenye mdomo wa kunywea, sikuyaamini macho yangu, nikataka kutema lakini tayari nilishachelewa, vitu vyote vilikimbilia tumboni vyenyewe.

Je, nini kitafuatia? Usikose next issue au bofya Simulizi za Majonzi kusoma mwendelezo.

Leave A Reply