The House of Favourite Newspapers

The Graves of The Innocents (Makaburi ya Wasio na Hatia)- 40

0

ILIPOISHIA:

Nilipokisogeza kibuyu hicho karibu na pua, nilikumbana na harufu kali kwelikweli, ikabidi nizibe pua, nikanywa huku nikiwa nimefumba macho. Kabla sijameza, nilisikia vitu vikinitembea mdomoni, nilipotazama vizuri kile kibuyu, pale kwenye mdomo wa kunywea, sikuyaamini macho yangu, nikataka kutema lakini tayari nilishachelewa, vitu vyote vilikimbilia tumboni vyenyewe.

SASA ENDELEA…

Pale kwenye sehemu ya kunywea, ndipo paliponipa picha kwamba nilichokunywa kilikuwa ni kitu gani. Minyoo mingi ya rangi mbalimbali, ilikuwa imechanganywa na maji machungu yenye harufu mbaya mno. Jambo lile, la kugundua kwamba nilikuwa nimekunywa minyoo, lilinifanya nisisimke sana, nilijaribu kujitapisha lakini ilikuwa sawa mna kazi bure.

Kwa jinsi minyoo yenyewe ilivyokuwa imechangamka, muda mfupi tu baadaye, nilisikia tumbo likianza kutibuka, hofu kubwa ikanitanda ndani ya moyo wangu. Sikujua nini itakuwa hatma yangu.

Yule babu alikichukuaa kibuyo na kukifunga, akakirudisha pale chini, nikamuona akichaguachagua na muda mfupi baadaye, alichukua kibuyu kingine lakini hiki kilikuwa kidogo kuliko kile cha awali. Akawatazama wale watu wengine waliokuwa wamekaa pembeni na kutulia kisha akawapa ishara fulani, nikaona wanaume wawili wakiinuka.

Wakatembea harakaharaka kusogea mpaka pale nilipokuwa nimekalishwa. Sikutaka kuyaamini macho yangu, ilibidi nijifikiche macho nikidhani labda nipo ndotoni.

Haikuwa ndoto, ilikuwa ni kweli kabisa. Mbele yangu walikuwa wamesimama baba na baba yake Rahma. Niliwatazama mmoja baada ya mwingine, bado nikawa siamini. Nao walikuwa wamevaa kama wale watu wengine, walijistiri kidogo tu lakini sehemu kubwa ya miili yao ilikuwa wazi.

Ni hapo ndipo nilipoielewa kauli ya baba yake Rahma aliyoitoa muda mfupi kabla ya yale mauzauza hayajanitokea, kwamba eti utii ni jambo muhimu sana na la lazima kwa jamii yao. Kumbe urafiki au ukaribu wa baba na baba yake rahma ulikuwa zaidi ya vile kila mmoja alivyokuwa akiamini.

>>Usiache kutembelea Simulizi za Majonzi

Yule mzee alimtazama baba, baba naye akamtazama kisha kichwa chake akakiinamisha kwa utii, yule babu akawa anaongea kwa lugha ambayo hata sikuwa naielewa, baba naye akawa anamfuatisha anachokisema, muda mfupi baadaye baba yake Rahma naye alikuwa akifuatisha walichokuwa wanakisema.

Muda mfupi baadaye, walinizunguka na kutengeneza kama duara jingine hivi, wakawa wanaendelea kuzungumza yale maneno kwa sauti ya juu, muda mfupi baadaye wale watu wengine nao walidakia, wakawa wanawafuatisha. Ilivyoonesha, wote walikuwa wakiielewa vizuri lugha ile maana hakuna aliyekuwa akibabaika.

Baadaye, yule mzee alitoa ishara, watu wote wakanyamaza, akaanza kuzungumza lakini safari hii, alikuwa akiongea Kiswahili japo ilionesha hakuwa akikielewa vizuri. Akawaambia watu wote kwamba anayo furaha kubwa kukutana nao usiku huo na furaha yake iliongezwa zaidi na tukio lililokuwa likifanyika usiku huo.

Aliwaambia watu wote kwamba kulikuwa na utambulisho wa mwanachama mpya, akanitaka nisimame. Nilishtuka sana, mwanachama mpya? Wa nini? Ina maana kile ni chama? Kinahusika na nini? Sikuwa na majibu. Nilimgeukia baba, naye akanigeukia, akanipa ishara kwamba nitulie.

Yule babu alimkabidhi baba kile kibuyu, nikamuona akirudi tena pale palipokuwa na vifaa vingine, akachaguachagua kisha nikamuona akichukua kitambaa cheusi, au wengine wanapenda kuita kaniki. Alimpa baba, akainamisha kichwa chake kama ishara ya utii, kisha yule babu akaendelea kuzungumza na kila mtu.

Alisema hatua ya kwanza natakiwa kukabidhiwa vifaa kwa ajili ya kazi kisha baada ya hapo, nitatawazwa rasmi kuwa mwanachama kamili, watu wote wakalipuka kwa shangwe za kila namna. Zilikuwa ni kelele kubwa sana, kila mtu akionesha kuwa na furaha sana.

Baba aliniinamia, akaongea kwa sauti ya chini akiniambia nivue suruali niliyokuwa nimevaa maana mpaka muda huo nilikuwa kifua wazi. Niliona kama ni jambo lisilowezekana, yaani nivue nguo wakati watu wote wananitazama? Macho yakanitoka.

>>Usiache kutembelea Simulizi za Majonzi

Ni kama baba alinielewa, alinipa na ile kaniki, akanionesha kwa ishara kwamba nijifunge juu ya suruali kisha ndiyo niiteremshe. Nilifanya hivyo, muda mfupi baadaye, nilikuwa nimeshaivua na kujifunga kaniki. Sasa na mimi nilikuwa nikifanana na wale watu isipokuwa mimi nilijifunga kaniki ndefu wakati wengine wote walikuwa wamejifunika kwa vipande vidogo.

Nilikalishwa chini, yule babu akampa ishara baba, akanisogelea na kupiga magoti, akanikabidhi kile kibuyu kilichokuwa kimevalishwa shanga, kisha akaongea kwa sauti ya chini akinitaka nisiogope chochote na nimthibitishie kwamba kweli nimekuwa mtu mzima na si mtoto kama alivyokuwa akiamini. Nilitingisha kichwa, japokuwa hakuwa ameniambia chochote, tayari nilishaelewa kilichokuwa kinaendelea.

Nilipokabidhiwa kile kibuyu, baba na baba yake Rahma waliondoka na kurudi kwenye sehemu zao, yule babu akaniambia nishike kibuyu hicho kwa mikono miwili kisha nikiinue mbele ya uso wangu.

Nilifanya kama alivyoniambia, nikamuona akichukua karai la chuma lenye maji meusi ndani yake, akanimwagia kichwani kisha kwa kutumia kisu kikali, alianza kuninyoa nywele. Sikuwahi kuona mtu akinyolewa nywele kwa siku, hata kule kijijini kwetu ambako saluni zilikuwa chache, tulikuwa tukinyolewa kwa wembe au mkasi.

Kwa kawaida nywele zangu huwa ni nguvu na wakati wa kunyoa huwa ni shughuli kwelikweli lakini huwezi kuamini, yule babu alipitisha mara kadhaa tu, kichwa kikawa cheupe kabisa. Alichukua dawa kutoka kwenye kichupa kimoja kisha akanisogelea, akarudia kunisisitiza kwamba sitakiwi kuachia kibuyu hicho kwani ndiyo maisha yangu.

Alichokifanya, kwa kutumia kilekile kisu, alianza kunichanja chake, kuanzia kichwani, akaja shingoni upande wa nyuma, akashuka mgongoni mpaka miguuni. Kiukweli maumivu niliyokuwa nayasikia yalikuwa makali sana, yote tisa, kumi ni pale alipoanza kunisugua sehemu alizonichanja kwa kutumia ile dawa iliyokuwa kwenye kile kichupa.

Maumivu ya kuchanjwa ukijumlisha na ukali wa ile dawa, nilishindwa kujizuia, nikawa nalia kwa maumivu.

“Kumbe hujakuwa mrume wewe,” alisema yule babu kwa Kiswahili kibovu lakini ambacho kilinifanya nimuelewe. Alimaanisha kwamba eti bado nilikuwa mtoto ndiyo maana nilikuwa nalia. Hakuna kitu ambacho nilikuwa nakichukia kama kuitwa mtoto. Japokuwa nilikuwa nikijisikia maumivu makali, ilibidi nijikaze, akaendelea kunisugua na ile dawa huku nikigugumia kwa maumivu.

Damu nyingi ilikuwa ikinitoka kwenye majeraha yangu lakini safari hii sikujali, sikutaka kuonekana mtoto, yule babu akaendelea mpaka alipomaliza. Baada ya kumaliza, alinishika mkono na kunisimamisha, akanisogeza kwenye ule moto.

Ni hapo ndipo nilipogundua kwamba kumbe pale kulikuwa na nyama nyingi ya kutosha imewekwa pembeni ya moto. Yule babu aliinama pale kwenye nyama, akatoka na kipande kimoja, akanifuata na kunipa.

Kwa akili yangu nilielewa kwamba ananipa ili niichome kwenye moto ikiiva ndiyo niile, nikashangaa ananiambia eti niile vilevile ikiwa mbichi. Nilishtuka sana maana ilikuwa bado na damudamu kabisa.

Nilitamani kumuuliza kwanza ile ni nyama ya nini lakini nilikumbuka kauli ya baba yake rahma na aliyoniambia baba muda mfupi uliopita kwamba natakiwa kuwa mtiifu, ikabidi nifumbe macho, nikaitia mdomoni na kutaka kuimeza bila kutafuna lakini ilikuwa kubwa, ikabidi nipige moyo konde, nikaanza kuitafuna kisha harakaharaka nikameza.

“Twive umile,” alisema yule mzee huku akinionesha kwa ishara kwamba nifumbue mdomo. Sijui kile ni kilugha alichokuwa akizungumza, nilifanya kama alivyoniambia, nikafumbua mdomo. Nadhani alitaka kuhakikisha kama nimemeza, alipohakikisha, alinishika mkono na kuuinua juu kama wanavyofanya waamuzi wa mapambano ya ndondi wanapomtangaza msshi ulingoni.

Watu wote walishangilia kwa nguvu, wengine nikawaona wakirukaruka kwa furaha, ikabidi na mimi nifurahi ingawa bado nilikuwa gizani. Yule mzee aliniachia mkono na kuanza kuzungumza na wale watu, akiwataka wanipe ushirikiano na kunifundisha yale nisiyoyajua.

Wakati anaongea hayo, sijui nini kilinituma nitazame pale zilipokuwepo zile nyama, nikashtuka kuliko kawaida kuona kuna viungo vya binadamu, viganja vya mikono na miguu. Ile nyama aliyonipa aliichukua palepale, kwa hiyo alikuwa amenipa nyama ya mtu? Macho yalinitoka nikiwa siamini macho yangu.

Nikiwa bado nashangaa, mwili ukiwa unatetemeka kwa hofu, nilishtukia wale watu wakikimbilia pale kwenye moto na kujipanga foleni, yule babu akasogea kwenye zile nyama, akawa anagawa, kila mmoja anapita na kupewa kipande chake kisha anatafuta sehemu ya kwenda kukaa na kuanza kula. Nilihisi kama nipo ndotoni lakini haikuwa hivyo.

“Hongera, umekuwa sasa,” alisema baba huku akinikumbatia, akanishika mkono na kunipeleka kwenye foleni, akaniingiza kwenye foleni.

Je, nini kitafuatia? Usikose next issue au bofya Simulizi za Majonzi.

Leave A Reply