Harry Kane Aomba Kuondoka Tottenham Hotspur
STAA wa Tottenham Hotspur, Harry Kane, ameshawaambia mabosi wa klabu hiyo kuwa anataka kuondoka mwishoni mwa msimu huu.Mshambuliaji huyo mwenye thamani ya pauni milioni 150, amekuwa akiwindwa na timu kadhaa kubwa za Ulaya msimu huu.
Staa huyo anawindwa na timu za Man City, Man United na Chelsea ingawa Spurs wenyewe wamekuwa wakisema kuwa hawataki kumuuza kwenye Ligi Kuu England.Staa huyo amewaambia mabosi wa timu hiyo kuwa anataka kufahamu mustakabali wake kabla ya michuano ya Euro ambayo itaanza baadaye mwezi ujao.
Mshambuliaji huyo amekuwa akisema kuwa anataka kwenda kuitumikia timu ambayo inashiriki michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya.
Manchester United walikuwa wa kwanza kutajwa kuwa wanamtaka mshambuliaji huyo mahiri na walikuwa wameshaweka kitita cha pauni milioni 100 mezani.
Hata hivyo, inaelezwa kuwa Spurs walikataa kitita hicho wakitaka pauni milioni 150.Gazeti la Daily Mail la Uingereza, limesema kuwa mbali na timu hizo pia timu za Paris Saint-Germain na Real Madrid, zinataka saini ya mchezaji huyo.