Hatimaye Mwili wa Shinzo Abe, Waziri Mkuu wa Zamani wa Japan Wazikwa Jijini Tokyo
WAZIRI Mkuu Mstaafu wa Japan, Shinzo Abe aliyeuawa kwa kupigwa risasi Ijumaa iliyopita, amezikwa leo jijini Tokyo.
Maelfu ya waombolezaji, wamekusanyika katika mitaa mbalimbali ya Jiji la Tokyo kutoa salamu zao za mwisho kwa mwili wa Abe, ambao ulipitishwa ukiwa kwenye gari maalum na kupelekwa kwenye Hekalu la Zojoji.
Baada ya kufikishwa kwenye hekalu hilo, ndugu, jamaa na marafiki pamoja na viongozi mbalimbali, nao walipata nafasi ya kutoa salamu zao za mwisho.
Mjane wa marehemu, Akie Abe, 60, ameonekana akiwa amebeba kibao maalum chenye wasifu wa marehemu, akiwa amekaa siti ya mbele ya gari lililobeba mwili wa mumewe huyo.
Baada ya kutoka katika hekalu hilo, mwili huo ulipelekwa katika Makaburi ya Kirigaya Funeral Hall ambako ulichomwa kama tamaduni za Wabudha zilivyo.
Shinzo Abe aliuawa kwa kupigwa risasi Ijumaa ya Julai 8, 2022, wakati akihutubia mkutano wa hadhara katika Mji wa Nara kwa lengo la kuwapigia kampeni wagombea wa chama kilichopo madarakani cha Liberal Democratic Party (LDP) katika uchaguzi uliokuwa ukitarajiwa kufanyika Jumapili ya Julai 10, siku mbili tu baadaye.
Aliyempiga risasi, ni Tetsuya Yamagami ambaye muda huohuo alikamatwa na wanausalama na kuwekwa nguvuni huku uchunguzi kuhusu tukio hilo ukiendelea.