The House of Favourite Newspapers

Hitilafu ndani ya kizazi “Endometriosis”-2

0

Blausen_0349_EndometriosisWiki iliyopita nilianza kulizungumzia tatizo hili na leo nitaimalizia ili wiki ijayo nianze mada nyingine.

JINSI YA KUJIKINGA NA TATIZO

Kila mwanamke aliye katika umri wa kuzaa anaweza kupatwa na tatizo hili. Mwanamke aliye katika umri wa kuzaa ni kuanzia msichana aliyevunja ungo hadi yule mama aliyefikia ukomo wa hedhi.

Kwa hiyo njia za kujinasua usipatwe na tatizo hili ni kuwa na tabia ya kufanya mazoezi ya mwili mara kwa mara, kuepuka kunywa pombe kupita kiasi na ikibidi acha kabisa au kama unapendelea kunywa basi hakikisha unatumia muda wa kutosha kufanya mazoezi mfano kuruka kamba, kukimbia au kutembea mwendo mrefu muda wa jioni.

UCHUNGUZI

Tatizo hili huchunguzwa hospitali katika hatua za awali, vipimo vya damu vitafanyika kuangalia mfumo wa homoni, maambukizi na wingi wa damu kama unatokwa sana na damu. Kipimo cha ‘Ultrasound’ kitathibitisha tatizo hili lakini ikibidi daktari ataangalia vipimo zaidi.

Ni vizuri umuone daktari wa akina mama katika hospitali ya mkoa kwa uchunguzi wa kina.

MATIBABU

Ugonjwa wa ‘Endometriosis’ huwa hautibiki, lakini zipo dawa zitakazokusaidia kupunguza kasi ya ugonjwa na ikibidi dawa za ‘Hormone’ zitatolewa, unaweza kufanyiwa upasuaji ikiwa tatizo litakuwa kali sana.

Upasuaji wa tumbo utasaidia kupunguza ugonjwa kusambaa ndani zaidi, mojawapo ni kutolewa kizazi.

Athari nyingine zinazotokea kwa mwanamke mwenye tatizo hili ni maumivu ya njia ya mkojo mara kwa mara, hulalamika akikojoa mkojo unauma kila akitumia dawa tatizo hujirudia.

Anaweza kuharisha kidogokidogo mara kwa mara au hata kufunga kupata choo hata kwa siku tatu.

Pia epuka kujamiiana ukiwa kwenye siku zako za hedhi au unapokaribia kabisa au damu kabla haijaisha vizuri kwani unaweza kupata hali iitwayo ‘Retrograde menstruation’.

Hapa damu ya hedhi badala ya kutoka nje ukeni inaendelea kutokea kwa ndani kupitia kwenye mirija ya uzazi.

Tatizo hili siyo tu linatokea katika mazingira haya lakini pia linaweza tu kujitokeza kwa bahati mbaya kwa mwanamke yeyote kutokana na mfumo wake wa mwili.

Leave A Reply