The House of Favourite Newspapers

Hitimana Bado Hakijaeleweka Simba

0

KOCHA Msaidizi wa Simba, Mnyarwanda, Thierry Hitimana, mpaka juzi Jumamosi ishu yake ya kupata vibali vya kazi ilikuwa haijakamlika.

 

Hitimana ambaye alitangazwa kuwa kocha msaidizi wa Simba hivi karibuni, bado hajakaa kwenye benchi la timu hiyo kutokana na kukosa vibali vya kazi, huku Simba ikiwa tayari imecheza mechi tatu za kimashindano.

 

Taarifa za uhakika kutoka ndani ya uongozi wa Simba, zinasema kwamba suala la Hitimana kupata vibali ambavyo vitamruhusu kukaa kwenye benchi la timu hiyo litajulikana baada ya timu kurejea Dar ikitokea Dodoma ilipocheza dhidi ya Dodoma Jiji.

 

“Mwalimu Hitimana suala lake la vibali vya kazi bado halijapatiwa ufumbuzi kwa sababu alikuwa akisubiri viongozi warudi Dar na timu wakitokea Dodoma tulipokwenda kucheza na Dodoma Jiji.

 

“Timu imerudi Dar leo (jana) kwa ajili ya maandalizi ya Ligi ya Mabingwa Afrika, baada ya wao kufika naamini itajulikana kila kitu kuhusiana na suala la kocha huyo na pengine mambo yakawa mazuri kabla ya mchezo wa kimataifa,” alisema mtoa taarifa.

 

Spoti Xtra lilimtafuta kocha huyo katika kujua hatima yake ya kupata vibali vya kazi, alipopatikana alisema kwa sasa hawezi kusema lolote kwa kuwa suala hilo linashughulikiwa na uongozi wa timu.

 

Kuna uwezekano mkubwa kocha huyo kazi yake ya kwanza ndani ya Simba ataanza dhidi ya Jwaneng Galaxy ya Botwasana katika mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika hatua ya kwanza. Simba ambayo itaanzia ugenini, mechi ya kwanza itachezwa Oktoba 15, mwaka huu, kabla ya marudiano Oktoba 22.

IBRAHIM MUSSA, DAR

 

Leave A Reply