The House of Favourite Newspapers

HIVI NDIVYO LULU ANAVYOISHI GEREZANI!

0

 

Msanii wa filamu Bongo, Elizabeth Michael ‘Lulu’.

PAMOJA na ustaa wake, msanii wa filamu Bongo, Elizabeth Michael ‘Lulu’, anadaiwa kuishi maisha ya tofauti kwa sasa kiasi cha kuwafanya watu waliozoea kumuona akiwa uraiani wamhurumie. Lulu anatumikia kifungo cha miaka miwili gerezani kutokana na kusababisha kifo cha aliyekuwa mpenzi wake, Steven Kanumba maarufu kama The Great.

TUJIUNGE NA CHANZO Kwa mujibu wa chanzo kilichokwenda kumjulia hali Lulu gerezani, mrembo huyo ameamua kufanya mambo yafuatayo katika kipindi chote cha kifungo chake ili kumuondolea msongo wa mawazo na aweze kutoka salama.
KUSALI Chanzo hicho kilisema, anachofanya Lulu kwa sasa ni kuhakikisha anatumia muda mwingi kusali kumuomba Mungu wake amsaidie atumikie kifungo chake na kumaliza salama. “Ameniambia kuwa hakuna kipindi ambacho anasali kama sasa kwani anaona kuwa karibu na Mungu ndiyo suala muhimu kwake,” kilisema.

MAZOEZI Chanzo hicho kilizidi kuweka bayana kuwa, pamoja na kufanya sana maombi, mrembo huyo kwa sasa amejikita katika suala zima la kufanya mazoezi ambayo kimsingi yanamfanya aondokane na mawazo mbalimbali hususan anapokumbuka maisha ya uraiani. “Muda mwingi anautumia gerezani kufanya mazoezi mbalimbali ya mwili. Alinieleza hata hivyo hafanyi hivyo kwa vile tu yupo gerezani bali ni utamaduni wake hata alipokuwa uraiani lakini kwa kule mazoezi yanamsaidia sana,”kilisema.

 

KUSOMA VITABU

Ukiachana na mazoezi na kusali, chanzo hicho kilieleza kuwa mara nyingi amekuwa
akijisomea vitabu mbalimbali na kuangalia vipindi kwenye televisheni hususan siku ambazo wanaruhusiwa kufanya hivyo. “Mambo haya manne aliniambia anayazingatia mno kwani yanamfanya asifikirie sana maisha ya uraiani na asiwaze kuhusu urefu wa kifungo chake cha miaka miwili, yanamsaidia sana kwa sasa,”kilifafanua.

 

ANA GENGE LA KUFANYA KAZI

Chanzo hicho kilizidi kueleza kuwa, ratiba ya Lulu imebana sana gerezani humo kwani mbali na kufanya hayo yote ya binafsi, bado mrembo huyo anatumikia ‘genge’ maalum la kufanya kazi za gerezani ambalo amepangiwa.

 

MAMA LULU ANASEMAJE?

 

Kwa upande wake, mama yake Lulu, Lucresia Karugila alipoulizwa na Amani kuhusu maisha ya mwanaye gerezani, hakutaka kuingia kwa undani. “Mmeanza mambo yenu…
,”alisema na kukata simu.

 

OFISA GEREZA

 

Amani lilifanikiwa kuzungumza na ofisa mmoja wa gereza ambaye hakupenda kutaja jina lake sababu si msemaji, ambapo alisema suala la Lulu kubadili mfumo wa maisha kwa gerezani haliepukiki. “Unajua huyu (Lulu) ni mwigizaji na amezoea kujichanganya na watu wengi, lakini kwa sasa hawezi kufanya hivyo…,” alisema.

 

TUMEFIKAJE HAPA? Itakumbukwa kuwa hukumu ya Lulu kutumikia adhabu hiyo ilitolewa na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Sam Rumanyika baada ya mahakama kujiridhisha aliua bila kukusudia.

 

TUJIKUMBUSHE

 

Kanumba alipoteza maisha Aprili 7, 2012, baada ya kutokea ugomvi kati yake na Lulu majira ya usiku wakiwa nyumbani kwa marehemu, Sinza-Vatican, jijini Dar es Salaam. Kanumba alijizolea umaarufu mkubwa katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati hadi Afrika Magharibi baada ya kuwashirikisha katika filamu zake baadhi ya wasanii maarufu wa kutoka nchini Nigeria, akiwemo Mercy Johnson na Ramsey Nouah.

 

KUZALIWA

 

Kanumba alizaliwa mwaka 1984 na kuanza kujipatia umaarufu mwanzoni mwa mwaka 2000 wakati huo akiigiza kupitia kundi la maigizo la Kaole Sanaa. Aliendelea kuigiza filamu nyingi ambazo zilimpatia umaarufu mkubwa hivyo kusafiri mara kadhaa nchi za nje, ambako alitambulika kama mmoja wa wasanii wenye vipaji vikubwa ambaye aliitangaza fani ya filamu nchini ‘Bongo Movies’.

 

MAZISHI Mazishi yake yalichukua sura ya kitaifa kutokana na umaarufu aliojijengea msanii huyo katika jamii ya Watanzania na hata nchi za nje.

STORI: GAZETI LA AMANI

Leave A Reply