The House of Favourite Newspapers

HIVI NDIVYO MAKONDA ALIVYOTAKA ‘KUUA’

 

DAR ES SALAAM: Mkuu wa Idara ya Ardhi, Wilaya ya Ilala jijini Dar es Salaam, Paul Mbembela, mwishoni mwa wiki iliyopita alinusurika kufa baada ya kubanwa maswali na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, Uwazi linakueleza jinsi ilivyokuwa.

Mbembela alipatwa na mshtuko na kuzimia ghafla kwenye mkutano huo maalum uliohusisha wananchi, wakuu wa idara zote za Jiji la Dar es Salaam pamoja na wanasheria katika Ukumbi wa Diamond Jubilee.

 

Mshutuko huo ulitokea mara baada ya Makonda kumuagiza Mkurugenzi wa Ilala amtafutie kazi nyingine baada ya kushindwa kueleza idadi kamili ya kesi za migogoro ya ardhi zilizopo katika idara yake zilizoshughulikiwa au kutatuliwa.

 

Makonda alisema kwenye ripoti aliyonayo, kuna malalamiko 1503 wakati Mbembela alisema anayo 139 tu kitendo ambacho kilimkasirisha Makonda na kutaka mkurugenzi amfute kazi mara moja hali iliyomfanya Mbembela azimie papo hapo na kukimbizwa Hospitali ya Amana.

 

Akizungumzia hali ya ofisa ardhi huyo, Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Sophia Mjema alisema kuwa alipata mshtuko, wakampeleka hospitali na hadi saa tatu usiku ya siku hiyo (Ijumaa), hali yake ilikuwa ikiendelea vizuri.

 

“Walivyomtoa pale ukumbini hali yake ilikuwa mbaya, ikabidi kumkimbiza katika Hospitali ya Amana kwa ajili ya kupatiwa matibabu,”alisema Mjema.

 

Hata hivyo, mbali na Mbembela aliyepoteza fahamu, mtumishi mwingine aliyevuliwa madaraka katika mkutano huo ni Khamis Songwe ambaye ni Mkuu wa Idara ya Ardhi Wilaya ya Ubungo.

 

DAKTARI ANENA

 

Akizungumza na Gazeti la Uwazi, Daktari maarufu jijini Dar, Godfrey Charles, alisema kitendo kilichomtokea kitaalam kinaitwa Neurogenic Shock ambapo ni aina ya mshtuko ambao ukimpata mtu unasababisha kushuka ghafla kwa msukumo wa damu ambao unasababisha kupungua kwa mapigo ya moyo.

 

Alisema kitendo hicho humtokea mtu baada ya kupata taarifa mbaya au nzuri. Alisema, mwili wa mwanadamu unapopata mshtuko huo, husababisha kushuka kwa msukumo wa damu, mapigo ya moyo nayo yanashuka na hewa inashindwa kufika kwenye ubongo na mtu kuweza kupata kiharusi.

“Madhara ya mshtuko huu yanaweza kumsababishia mgonjwa kupata kiharusi au kupoteza maisha kabisa,” alisema Dk. Charles.

 

STORI: MWANDISHI WETU, UWAZI

Comments are closed.