Stori: Daktari wa Uwazi, UWAZI
Tunamalizia kuelezea ugonjwa wa homa ya mapafu kwa watoto.
Dalili mojawapo ya mtoto kuwa na homa ya mapafu ni kutokuwa na hamu ya kucheza na kupoteza hamu ya kula na kushindwa kunyonya. Pia mtoto hubadilika rangi na kuwa na rangi ya bluu katika midomo na kucha.
Hata hivyo, si lazima dalili zote hizi ziwepo kwa kila mtoto. Baadhi ya watoto huonesha kupumua kwa haraka kama dalili pekee ya homa ya mapafu. Iwapo vimelea vimeshambulia sehemu za chini ya mapafu karibu ya tumbo, sehemu ijulikanayo kama kiwambo au Diaphragm, mtoto anaweza asioneshe hali yoyote ya kushindwa kupumua ingawa anaweza kuwa na homa na kuhisi maumivu makali ya tumbo, vichomi na pia kutapika.
VIPIMO NA TIBA
Kwa kawaida daktari humchunguza mtoto mgonjwa kwa kusikiliza dalili za ugonjwa kutoka kwa mzazi au mlezi wa mtoto na pia huchunguza viashiria vya ugonjwa huu na kisha kumpima kwa kutumia kifaa kinachosaidia kusikia sauti mbalim bali katika mfumo wa hewa wa mgonjwa kinachoitwa Stethoscope.
Ili kuwa na uhakika kwamba mgonjwa ana homa ya Pneumonia, vipimo vifuatavyo vinaweza kufanywa kulingana na mazingira na upatikanaji wake.
Vipimo hivyo ni pamoja na X-ray ya kifua, au CT-scan ya kifua, pamoja na damu ili kuchunguza madhara yaliyoletwa na homa hii ya mapafu.
Faida ya kipimo cha CT-scan ni uwezo wake wa kutofautisha aina tofauti za homa ya mapafu na aina ijulikanayo kama Atypical Pneumonia ambayo si rahisi kuonekana kwa kutumia X-ray ya kawaida ya kifua.
X-ray ya kifua na CT-scan ya kifua kwa pamoja vina uwezo wa kuonesha tatizo hata pale ambapo daktari ameshindwa kusikia sauti maalumu kwa kutumia kifaa chake cha Stethoscope.
Maamuzi ya matibabu kwa watoto wenye homa ya mapafu hutegemea aina ya vimelea, umri na hali ya mtoto. Mara nyingi dawa za Antibiotics ndizo hutumika katika kutibu homa ya mapafu inayosababishwa na maambukizi ya bakteria.
Kwa homa ya mapafu inayosababishwa na virusi, dawa za Antibiotics hazina uwezo wa kutibu.