Yanga Wakanusha Waarabu Kugomea Kirumba…
UONGOZI wa Klabu ya Yanga umekanusha taarifa za wapinzani wao wa Kombe la Shirikisho Afrika (Caf), Pyramids FC ya nchini Misri kugomea kutumia Uwanja wa CCM Kirumba wa mkoani Mwanza.
Hiyo ikiwa ni siku chache tangu uongozi wa Yanga utangaze kuuhamishia mchezo huo CCM Kirumba utakaopigwa Oktoba 27, mwaka huu saa kumi jioni. Yanga, awali ilikuwa ikitumia Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam katika michezo ya Ligi ya Mabingwa Afrika kabla ya kuhamishia Mwanza.
Makamu Mwenyekiti wa Yanga, Frederick Mwakalebela amelifunulia gazeti hili kuwa taarifa zinazodai wapinzani wao Pyramids kupeleka malalamiko Caf ikipinga mabadiliko ya uwanja waliyofanya siyo kweli.
“Hakuna malalamiko yoyote yaliyopelekwa na Pyramids, hivyo mchezo utachezwa Mwanza kama tulivyopanga awali, tunawafahamu wanaozusha hizo taarifa ni wapinzani hapa nchini.
“Ifahamike kuwa kabla ya kuanza mashindano kila timu ilitakiwa kuwasilisha viwanja viwili ambavyo watavitumia, sisi tuliwasilisha CCM Kirumba na Uwanja wa Taifa ambayo ndiyo viwanja rasmi kwetu,” alisema Mwakalebela.
Comments are closed.