The House of Favourite Newspapers

Ishu ya Yondani, Uongozi Yanga Wakubaliana na Zahera

UONGOZI wa Yanga umemaliza Sakata lililojitokeza hivi karibuni kati ya kocha mkuu wa timu hiyo raia wa DR Congo, Mwinyi Zahera na aliyekuwa nahodha wao, Kelvin Yondani.

 

Sakata hilo ni lile la Zahera kumvua Yondani unahodha wa timu hiyo na kumkabidhi majukumu hayo, Ibrahim Ajibu kutokana na kile alichodai kuwa ni kuchoshwa na vitendo vya utovu wa nidhamu vya beki hiyo.

 

Uamuzi wake huo ulionekana kutoungwa mkono na baadhi ya watu ambao waliona kuwa Zahera hakumtendea haki Yondani, lakini baada ya mvutano wa hapa na pele juu ya sakata hilo hatimaye uongozi wa Yanga umekubaliana na maamuzi hayo ya kocha wao huyo.

 

Habari za kuaminika kutoka ndani ya Yanga ambazo Championi Jumatatu limezipata zimedai kuwa, baada ya uongozi huo kupokea ripoti ya Zahera kuhusiana na mabadiliko hayo, umekubaliana na jambo hilo.

 

“Uongozi umehitimisha sakata hilo baada ya kukubaliana na maamuzi ya Zahera dhidi ya Yondani kwani baada ya kuipitia ripoti yake, umekubaliana na maamuzi hayo.

 

“Alichokisema katika ripoti hiyo kila mtu amekubaliana nacho na hakuna aliyepinga na wote kwa pamoja wametoa baraka zao juu ya hilo na kumtakia kazi njema Ajibu katika kuwaongoza wenzake,” kilisema chanzo hicho cha habari.

 

Alipoulizwa kuhusiana na hilo, Kaimu Mwenyekiti wa Yanga, Samwel Lukumay alisema: “Mwenye maamuzi ya nani awe nahodha wa timu ni kocha, kwa hiyo kama yeye kaamua kufanya mabadiliko ya nafasi hiyo hatuwezi kumpinga.

 

“Yeye ndiye anayekaa na wachezaji muda mwingi kuliko sisi na yeye ndiye anayejua tabia zao kwa hiyo katika hilo sisi hatuna la kusema ila tu tunamtakia Ajibu kazi njema ya kuwaongoza wenzake.”

Comments are closed.