The House of Favourite Newspapers

Jamani Antiii…Nishushe Ununio-10

ILIPOISHIA KWENYE RISASI JUMAMOSI:

Kwere aliondoka na kumuacha Bigambo akiwaza hili na lile kichwani mwake juu ya namna gani aanze kuishi na wale watu wa ofisini kwake. Ni kweli waliwahi kumuumiza kwa mambo mengi sana lakini kwa hili lilikuwa pigo kubwa kwani kumsemea kwa meneja kwamba ana uhusiano usiofaa na Vivian ilikuwa ni kumharibia kwa sehemu zote mbili. Kwamba anaweza kutimuliwa kazi na kumkosa Vivian ambaye alikuwa amemuonjesha penzi tamu kuwahi kupewa tangu aanze kujihusisha na masuala hayo.

Wakati Bigambo akiwazua hayo, ghafla simu yake iliita na alipoitazama kwenye kioo, ilikuwa namba ngeni na akaipokea harakaharaka na kuiweka sikioni huku akisikilizia ni nani alikuwa amempigia na alikuwa na ishu gani.

Mpigaji wa simu ile alikuwa Vivian, aliamua kumpigia kwa namba ngeni akiwa na maana kubwa sana.

“Enhe, imekuwa hivyo tena? Ayaa kwa nini Vivian? Yeye amekuambiaje?” Bigambo aliuliza kwa hamaki baada ya kuambiwa maneno f’lani na Vivian yaliyochoma moyo wake kwa ncha kali ya kisu chenye moto mkali.

SHUKA NAYO SASA…

BIGAMBO alihamaki mno. Maneno ya Vivian yalikuwa yamemuondoa kabisa kwenye mudi ya kufanya chochote. Alichokifanya ni kuzungumza na mmoja wa viongozi wake na kumuomba ruhusa ya kwenda nyumbani kupumzika akisingizia kichwa kinamuuma ingawa ukweli ni kwamba alikuwa na msongo mkubwa wa mawazo.

***

Baada ya kutoka kwa meneja, Vivian alikuwa amechanganyikiwa kupindukia. Tangu aanze kujihusisha na masuala ya mapenzi, hakuwahi kufikishwa kwa kiongozi wake wa kazi hata kabla ya kuanza kufanya kazi hapo. Aliifikiria aibu atakayokumbana nayo pale ofisini endapo suala la kuitwa kwa meneja litawafikia wafanyakazi wenzake.

“Lazima nifanye uamuzi mkubwa bila kujali utamuumiza nani na kwa kiwango gani, lazima niachane na Bigambo na sitaki tena kujihusisha na mapenzi na mfanyakazi mwenzangu kuanzia leo,” Vivian aliwaza huku akishika simu yake na kumpigia Bigambo kwa namba ambayo hakuwahi kumpigia nayo na kumueleza ukweli ambao alitarajia kukutana na lawama lakini hakujali sana kwani alikuwa ameamua kutoka moyoni kwamba ni lazima aachane na Bigambo.

Bigambo aliondoka akiwa na mawazo mengi kichwani mwake. Hakujua ataishije bila Vivian licha ya kwamba walikuwa na muda mfupi sana tangu wafahamiane na kupeana penzi mara moja, lakini mahaba ya mwanamke huyo kutoka Tanga yalimkolea sana kijana wa watu.

“Nitaishije mimi bila huyu mwanamke? Mimi ni kidume, nitambembeleza kwa kila njia kuhakikisha namuweka sawa tena kwenye himaya yangu, siwezi kuruhusu kirahisi hivi aniache, siwezi hata kidogo,” Bigambo naye alipangilia mawazo kichwani huku akidandia daladala, tayari kwenda nyumbani kujilaza ili apunguze mawazo.

Alilala hadi mchana ambapo aliwasha simu yake aliyokuwa ameizima tangu afike nyumbani. Meseji zilianza kumiminika moja baada ya nyingine kutoka kwenye mtandao ukimjulisha namba ambazo zilikuwa zimempigia akiwa amezima simu, namba ya Vivian ilikuwa miongoni mwa namba hizo.

“Mmmh,” Bigambo aliguna kwanza huku akishindwa kuamini kama ni kweli Vivian alikuwa amempigia tena licha ya kumwambia maneno ya kuachana tena kwa sauti kavu isiyokuwa na masihara hata chembe.

“Amenipigia kweli? Anataka kuniambia nini zaidi ya kuniumiza zaidi? Ngoja nimpigie nisikie tena anachotaka kuniambia lakini kama ni yaleyale ya kusisitiza kwamba ameachana na mimi sitampa nafasi ya kumsikiliza, sitaki maumivu tena nikiwa najiandaa kumrejesha, Bigambo aliwaza moyoni na kumpigia Vivian ambapo alikuta namba ikiwa inatumika, hivyo alilazimika kusubiri kwa muda.

Aliagiza chakula na wakati ananawa, simu yake iliita na alipoitazama aliona jina la My Vivian, kama alivyokuwa amelihifadhi kwenye orodha ya majina yake ya simu. Moyo ulimlipuka na kujikaza kiume ambapo aliipokea simu kwa nidhamu zote akijiandaa kusikia lolote kutoka kwa mwanamke huyo mrembo.

“Salama kabisa, nakusikiliza Vivian,” Bigambo aliharakisha ili kujua lengo la Vivian kumpigia tena simu.

“Nilikuwa nimelala ndiyo maana nikazima simu.”

Licha ya kujiapiza kwa dhamira ya kweli kwamba hataki tena mapenzi na mtu wa ofisini, moyo wa Vivian ulikuwa bado na hisia za kimapenzi kwa Bigambo, mwanaume ambaye alimuonesha upendo wa kweli kabisa na hata kwenye uwanja wa fundi seremala, alikuwa akijiweza vilivyo.

“Hapana, zilikuwa ni hasira hizo, naomba tuonane tuzungumze tena ili tuone tunafanyaje, tafadhali naomba my love, nakupenda sana Bigambo nimeulizia nikaambiwa umeomba ruhusa ya kwenda nyumbani kwa kuwa unaumwa kichwa, naomba nije nikuone mpenzi wangu, nakuja sasa hivi nikifika hapo Riverside nitakupigia unielekeze nyumbani kwako,” Vivian alisema mfululizo bila kumpa Bigambo nafasi ya kusema chochote na kisha kukata simu, jambo ambalo lilimuacha njia panda kijana wa watu.

“Duh! Huyu demu kiboko aisee, mbona hii ni ajabu sana? Yaani ametoka kunitamkia maneno makali muda siyo mrefu akinitaka niachane naye halafu sasa hivi anataka tuzungumze tena na anadai ananipenda sana, mapenzi ni kitu cha ajabu sana jamani,” Bigambo alijisemea moyoni huku akifurahi kimyakimya.

Dakika 45 baadaye, simu ya Bigambo iliita tena na alipoitazama mpigaji alikuwa ni Vivian, akatabasamu na kuipokea haraka sana.

“Umefika? Basi njoo hadi pale pa siku ile nitakufuata nikupeleke nyumbani,” Bigambo alijibu na kuanza kujisogeza kwenye ile baa waliyokaa na Vivian kwa mara ya kwanza walipokutana kwa ajili ya mazungumzo na kuishia kufanya kweli.

Vivian alitembea kwa haraka, moyoni akiwa na shauku ya kumuona tena Bigambo. Nafsi ilikiri kabisa kwamba alimpenda mno mwanaume huyo, ingawa walikuwa na muda mfupi tangu wakutane. Muda mfupi alifika na kumfahamisha Bigambo ambaye alifika na kumchukua hadi nyumbani kwake.

“Pole kwa kuumwa na kichwa baba,” Vivian alianza mazungumzo kwa maneno hayo huku akimshika kichwani Bigambo, ambaye alibaki ametulia kimya bila kupinga chochote.

“Lakini Vivian, mbona umeniumiza sana moyo leo, ni kwa nini uliamua kunieleza maneno makali namna hiyo?” Bigambo naye alijibaraguza ingawa moyoni alifurahia sana kitendo cha Vivian kumtafuta na hatimaye kukaa pamoja, tena ikiwa chumbani kwake.

“Tuachane na hayo baba, ndiyo maana nimekuja tuyamalize, unajua maneno ya meneja yalinichanganya sana na kujikuta nikijawa na hasira kali lakini baada ya kutafakari kwa kina nimegundua kwamba nakupenda sana mpenzi wangu na kamwe siwezi kuishi bila penzi lako, nisamehe kwa kukuumiza baba yangu, sitarudia kweli tena,” Vivian alisema huku akimpapasa Bigambo kichwani na kuyachezea masikio kwa kuyaminyaminya na kuyakanda, kitendo kilichoanza kuamsha hisia za mambo f’lani kwa Bigambo.

“Sawa, nimekuelewa lakini siku nyingine tusiumizane hivi bwana, sawa mama?” Bigambo alisema ingawa sauti yake ilitoka kwa tabu kutokana na kuanza kuelemewa na mahaba mazito.

Ili kutoonekana goigoi au mshamba wa mambo hayo, Bigambo naye alianza kujibu mashambulizi kwa Vivian. Alipeleka mkono wa kulia shavuni kwa Vivian na kuanza kupapasa taratibu lakini hakuishia hapo na badala yake alihamishia kiganja shingoni na kuwa kama anacharaza gitaa, kufikia hapo Vivian akaanza kufumba na kufumbua macho kwa tabu kama anayenyemelewa na usingizi mzito.

“Oooh, baba jamani,” Vivian alianza kulalamika na kujikunjakunja huku naye akiendelea na zoezi la kupashana joto. Ilifika mahali mpambano ulikolea na kwa pamoja wakajikuta wakiwa hoi na kilichoendelea kilimtosha kila mmoja wao.

Mtanange aliouonesha Bigambo kwa Vivian haukuwa wa nchi hii. Alifanya kwa makusudi ili arejeshe adabu na kweli alifanikiwa kwani alifanya kwa kiwango ambacho hata yeye alishangaa mno.

Baadaye walipitiwa na usingizi mzito ambapo walishtuka ikiwa ni saa mbili kasoro dakika kadhaa usiku. Bigambo akitarajia baada ya kukurupuka, Vivian angeanza harakati za kuondoka, lakini ndiyo kwanza mama wa watu akaendelea kujilaza huku akijibaraguza kwa maneno yasiyokuwa na msingi wowote.

“Niambie my love,” Vivian alisema huku akimshika Bigambo kichwani na kuzichezea nywele ambazo zilikuwa zinaanza kuota kwa mbali.

“Nakusikiliza mama yangu,” Bigambo alijibu akitarajia kusikia neno la ‘nataka kuondoka’ kutoka mdomoni kwa Vivian, lakini alichokisikia ni kingine kabisa.

“Tunakula nini usiku huu kabla ya kulala mume wangu?’ Vivian aliuliza swali ambalo Bigambo hakulitarajia kabisa na kujikuta akitabasamu.

“Wewe unataka tule nini?” Bigambo naye alimuuliza.

“Nakusikiliza wewe baba.”

“Kwani unalala hapa?” Bigambo aliamua kutoa dukuduku lake.

“Ndiyo mume wangu au hupendi nilale na wewe jamani, sema basi niondoke?” Vivian alisema na kuinuka kabla ya kukaa sawa kitandani na kumtazama Bigambo kwa jicho la kusikilizia jibu lake.

Kabla Bigambo hajajibu chochote, ilisikika sauti ya jirani wao ikimuita Bigambo.

“Wewe Bigambo wewe?”

“Naam.”

“Njoo kuna mgeni huku nje.”

“Ni nani huyo?”

“Wifi amekuja,” sauti ya nje ilisikika na hapohapo Vivian akamtazama Bigambo kwa hamaki huku akishindwa kuamini alichokisikia.

Je, ni wifi gani tena huyo? Usikose kufuatilia siku ya Jumamosi kwenye Gazeti la Risasi. 0673 42 38 45.

NA IRENE MWAMFUPE NDAUKA

Comments are closed.