The House of Favourite Newspapers

Jamani Antiii…Nishushe Ununio..!-5

0

ILIPOISHIA RISASI MCHANGANYIKO:

“Hapana, hebu ngoja kwanza nitengeneze ndipo nikuambie ni kiasi gani maana kwa sasa naweza kusema kumbe nikawa nimekupiga sana au umenipiga, kazi ikikamilika nitapima na kisha kukupa bei yangu, lakini naamini kabisa haitakuwa kubwa.”

“Sawa, ngoja nichukue bia moja au mbili hapo jirani nijipoze kidogo maana kwa varangati hili dah,” alisema Vivian akimtazama fundi.

“Kwani kimetokea nini Anti, maana sikuwepo nyumbani na nimerudi muda huu na kusimuliwa kwa juujuu tu,” fundi aliuliza.

“Wewe acha tu, nyie wanaume mna maana nyie basi,” alisema Vivian.

“Sasa ukisema hivyo utakuwa umekosea.”

“Basi nitakuja kukusimulia nikirudi, wewe unakunywa bia gani nikuletee japo mbili za kutuliza koo lako?”

“Mimi anti huwa sinywi bia zaidi ya Nyagi tu,” fundi huyo ambaye jina lake halisi aliitwa Jisu alisema huku akimtazama Vivian kwa macho ya kudadisi atasema nini.

“Mmmh, basi sawa ngoja nikakuletee kubwa moja kabisa ili uburudike vya kutosha, unachanganya na soda au maji?”

“Vyovyote hata kavu huwa napiga,” alisema Jisu na kumnfanya Vivian acheke na kuondoka kwenda kwenye grosari.

SEREREKA NAYO SASA…

HUKU nyuma, spidi ya fundi kutengeneza mlango iliongezeka maradufu, kitendo cha Vivian kufuata Nyagi kilimpa furaha isiyo kifani.

“Dah, huyu sista amewaza kikubwa mlemle aisee, kajuaje kama nina hamu sana na Nyagi leo, ila sema tatizo ni moja kwamba wifi yake amesafiri na raha ya Nyagi ni kucheza mechi ya kukata na shoka,” Fundi Jisu aliwaza huku akikomelea msumari kwenye komeo ambalo tayari lilishakaa sawa.

Dakika mbili baadaye, mlango wa Vivian ulikuwa sawa kabisa na sasa Jisu alikaa pembeni kwa nje akimsubiri mwenyeji wake aje wamalizane kwa ujira kama si kupiga masanga ambayo atakuwa ameyaleta Vivian.

Vivian alirejea, mkononi alikuwa ameshika mfuko mweusi ambao ulikuwa umeelemewa na mzigo uliokuwemo ndani. Jisu kuona vile, mate ya ulevi yakaanza kujitengeneza mdomoni.

“Vipi fundi.”

“Poa tu sista.”

“Mbona umekaa.”

“Nimemaliza kazi.”

“Wee, mara hii?”

“Ndiyo sista, huamini au?

“Hata siamini,” alisema Vivian na kupiga hatua za haraka hadi mlangoni ambapo hakuwa na haja ya kumulika kwani mwanga wa umeme ulitosha kabisa kumulika mahali pote. Aliushika mlango na kuutikisa vyema ambapo alijiridhisha kabisa kwamba ulikuwa umetengemaa na uko tayari kwa matumizi, akatabasamu na kumgeukia fundi.

“Aisee, wewe ni kiboko fundi jamani.”

“Kwa nini sista?”

“Umefanya haraka sana.”

“Kawaida, watu husema kazi ukiizoea yanakuwa maisha yako ya kila siku,” alisema Jisu huku akinyanyuka mahali alipokuwa ameketi na kumsogelea Vivian ambaye alikuwa ameshikilia mfuko wenye masanga.

“Vipi, umepata Nyagi?” Jisu aliuliza kwa hamu kubwa akichungulia ndani ya mfuko.

“Yeah, si tunakaa ndani jamani?”

“Hapana sista, hapahapa nje panatosha muhimu ni glasi na kazi ianze mara moja, nikizidiwa sana nitaenda kumalizia nyumbani kwangu,” alisema Jisu akimtazama Vivian usoni, aliishia kutabasamu bila kusema chochote.

Vivian aliingia ndani na kutoka na viti viwili na meza ndogo pamoja na glasi mbili, unaweza kushangaa alivibebaje vyote hivyo kwa wakati mmoja lakini huo ndiyo ukweli kwamba alivileta vyote kwa pamoja.

“Karibu tena mgeni kwa mara nyingine, jisikie uko nyumbani kabisa,” alisema Vivian akikaa vyema kitini na kumruhusu Jisu kwa ishara aungane naye waweze kuianzisha safari ya kulabuka, yaani kugida maji hayo machungu lakini yenye kuchangamsha ubongo kwa kasi ya haraka!

Vivian alitoa mfuko na kuchomoa Reds sita za chupa na mzinga mmoja mkubwa wa Nyagi na soda moja ambapo alivimwaga kwa pamoja.

Hapohapo, meno yote ya fundi yakaonekana kwa mpangilio yakinifu kabisa na bila kuchelewa akapeleka mkono wa kulia na kuishika glasi, awamu hii hakungoja tena karibu na badala yake akamimina Nyagi kidogo na kuchanganya na soda.

“Ngoja nipunguze mawazo miye,” alisema Vivian na kuchukua chupa moja ya Reds ambayo aliinywa kwa ule mtindo wa tarumbeta, yaani bila kutumia glasi. Walikunywa wakiwa kimyakimya, nusu saa baadaye kila mmoja alianza kujawa na ujasiri wa hali ya juu ambapo walitazamana usoni bila aibu.

Walianza kusimuliana jinsi ambavyo mapenzi yamekuwa yakimtesa kila mmoja wao. Vivian alimwaga siri zote na namna ambavyo huwa anajisikia raha pale anapokutana na mwanaume mwenye kuweza mambo.

“Mimi huwa najali sana kumwandaa mwanamke kabla mimi sijajiandaa, unajua raha ya tendo ni mwanamke kuanza kufika mwisho wa safari ndipo ampe sapoti mwanaume, hakika hilo huwa nalizingatia sana,” alianza kujinasibu Jisu bila kujua anaanza kumpa wakati mgumu Vivian ambaye akinywa pombe hususan Reds huwa mwepesi kushinda maharage ya Mbeya kama siyo kunde za Mlandizi na choroko za Mtwara!

Hali ya Vivian ilianza kubadilika lakini alijisitiri sana asionekane kama ni dhaifu kwa kiasi hicho na pia hakuwahi kuwaza kutoa penzi kwa mwanaume aina ya Jisu, ambaye hakuwa hadhi yake kabisa.

Vivian alikuwa na nyodo nyie acheni tu! Hata huo uchangamfu aliouonesha kwa Jisu ni kutokana na mvurugano uliotokea muda mfupi uliopita na kwa namna ambavyo fundi huyo amefanya kazi yake haraka na kwa ustadi wa hali ya juu, ukichanganganya na kimea cha kwenye Reds hapo mambo yanakuwa murua, lakini akiwa mkavu wa kawaida, unaanzaje kumkamata Vivian wewe mwanaume kapuku wa pangu pakavu, pangusa tukae?

“Kwa hiyo wewe fundi ni mtaalam sana kuhakikisha mwanamke anapata raha yake?” Vivian aliuliza akimtazama Jisu usoni kwa macho yenye kulegea kama mpishi aliyezidiwa na moshi wa kuni mbichi.

“Kabisa, tena kuna wakati huwa najikuta naongeza na utaalam ambao nikiambiwa nirudie siwezi kabisa, yote hayo ni kuhakikisha najitoa ufahamu kwenye sita kwa sita, hapo sasa nitagusa na maeneo ambayo wanawake wengi huwa hawaguswi mara kwa mara,” alisema fundi na kuendelea;

“Unajua kuna wanawake hawajawahi kupata raha ya tendo, ukiwaambia habari za kufika mwisho wa safari hawajui inazungumzia nini na wao wanakuambia wanafurahia mapenzi na waume zao, lakini kifupi ni kwamba hakuna mwanamke ambaye hana uwezo wa kufika mwisho wa safari, mwanamke yeyote ni maandalizi, akipata mwandaaji mzuri kabla ya mechi, ni lazima afike ukingoni tena kwa shangwe na makelele ya fujo kama siyo nderemo,” alisema Jisu huku akisukumizia maneno hayo na glasi ya Nyagi kabla hajakunja sura yake yenye mashimo kadhaa.

“Wewe Jisu wewe jamani,” Vivian alisema na kuiweka mezani kabisa chupa ya Reds aliyokuwa ameishika mkononi, licha ya kwamba kabla hajafika nyumbani alitoka kucheza gwaride na Bigambo, lakini maneno ya Jisu yalianza kumshawishi zaidi ya ufundi aliooneshwa na Bigambo, kichwani alianza kufanya tathmini na kuona wazi kabisa kwamba Jisu alikuwa mbobezi wa masuala ya chumbani kuliko Bigambo.

“Sasa kwa hiyo unaweza kumtibu mwanamke ambaye ana tatizo la kutofika mwisho wa safari yake?” Vivian aliuliza lakini awamu hii alishindwa kujizuia na kuuweka mkono wa kulia begani kwa Jisu, ambaye hakutoa upinzani wowote na zaidi sana akanyanyua glasi ya Nyagi na kuisukumizia mdomoni.

“Eee, sana tu, mimi nimetibu sana wanawake ambao shida yao ni kutofurahia na kufika mwisho wa safari, lakini nawatibu kwa vitendo bila kufanya nao kikwelikweli,” alisema Jisu na kuifakamia tena glasi yake ya Nyagi na kisha kumtazama usoni Vivian ambaye alikuwa kimya.

“Mmh,” Vivian aliishia kuguna na kuikamata chupa yake ya Reds.

“Vipi, mbona unaguna?”

“Mmmh, kawaida tu,” alisema Vivian na kuuondoa mkono wake begani kwa Jisu.

“Nikuombe kitu?” Vivian alianzisha tena mazungumzo.

“Sema tu sista.”

“Aaah, usiniite hivyo bwana,” Vivian alisema lakini sauti yake ilitoka kwa tabu na dalili za uchovu kwani pua zake zilikuwa zinabana kama mgonjwa wa mafua yenye kuambatana na malaria.

“Okey, samahani.”

“Unaweza kunitibu na mimi Jisu?” Vivian aliuliza na kumtazama tena usoni Jisu lakini pia akawa kama anayesikilizia jibu ambalo hakujua lingetokaje kwa wakati huo.

Hata hivyo, kabla Jisu hajamjibu Vivian alimimina tena Nyagi kwenye glasi na kuipiga yote kabla ya kumimina nyingine tena na kuiweka mezani bila kuinywa na hapohapo akanyanyuka kidogo na kukiweka sawa kiti chake ambapo sasa aligeukiana na Vivian, alimtazama usoni na wote wakawa wametazamana bila kupepesa macho na Jisu akapanua mdomo kama anayetaka kuuliza kitu kwa staili ya kipekee.

Je, nini kitaendelea? Usikose kufuatilia wiki ijayo siku ya Jumatano kwenye Gazeti la Risasi Mchanganyiko. Kwa maoni na ushauri nicheki kwa namba hizi; 0673 42 38 45.

Na Irene Mwamfupe

Leave A Reply