The House of Favourite Newspapers

JB, Ray, Rich Wabanwa Kuhongwa Viwanja

0

STORI: GLADNESS MALLYA NA ERICK EVARIST | RISASI MCHANGANYIKO

DAR ES SALAAM: Baada ya kuwepo kwa madai kuwa mastaa wa filamu Bongo, Jacob Steven (JB), Single Mtambalike (Rich) na Vincent Kigosi (Ray) walihongwa fedha na viwanja ili ‘kuinjinia’ maandamano ya hivi karibuni kupinga sinema za nje, mastaa hao wamebanwa na hatimaye kufungukia ishu hiyo inayowatafuna, Risasi Mchanganyiko lina mkanda kamili.

Chanzo kilicho karibu na tasnia hiyo kililiambia Risasi Mchanganyiko kuwa kampuni moja ya usambazaji filamu (jina kapuni kwa sasa), iliwapa fedha baadhi ya waigizaji ili wafanye maandamano ya kuziondoa sokoni filamu hizo za nje, zinazodaiwa kukingiwa kifua na Rais wa Shirikisho la Filamu Tanzania, Simon Mwakifwamba.

Single Mtambalike (Rich)

Inadaiwa kuwa baada ya kampuni hiyo ya usambazaji ‘kupenyeza sumu hiyo’ waigizaji hao walikwenda kwa kigogo mmoja wa kisiasa na kumshawishi kuwaunga mkono, ambaye naye alikubali na kuwaomba waigizaji hao kufanya kila wawezalo, kumtoa kwenye kiti chake, Simon Mwakifwamba, kwani ana ukaribu na hasimu wake wa siasa.

“Kuna watu wamevuta huku na huku katika hii ishu, wale wasambazaji hawazitaki kabisa filamu za ndani kwa sababu zinaharibu soko lao, ingawa wana kisingizio cha kodi, hawana lolote, watu hawataki sinema za Bongo kwa sababu hazina ubora,” kilisema chanzo hicho.

Kiliendelea kudai kuwa katika kuhakikisha lengo hilo linafanikiwa, kigogo huyo wa kisiasa anadaiwa kutoa hongo ya viwanja kwa mastaa hao, ambavyo vinadaiwa viko Kigamboni jijini Dar.

Ili kuujua ukweli juu ya tuhuma hizo, Risasi Mchanganyiko liliwatafuta waliotajwa na kuwabana ili wafungukie ishi hiyo.

Ray

Ray alipoulizwa alijibu akisema; “Hiyo ishu ya kupewa viwanja hainiingii akilini, kwanza ili iweje, mimi nilienda kwenye maandamano maana ni ishu iliyokuwa inanihusu kama msanii wa filamu, huyo Mwakifwamba ambaye anapinga suala hilo atakuwa ana mambo yake ya kisiasa, kwanza yeye mara ya mwisho kutoa filamu sijui ni lini.

“Sisi tunapigania haki yetu maana filamu za nje hazitozwi kodi, ndiyo maana zinauzwa bei rahisi kitu ambacho kinaathiri soko la filamu zetu nzuri na zenye ubora tunazozitengeneza.”

Kwa upande wa JB alipoulizwa kuhusiana na hilo alijibu; “Ili iweje? Kwani (anamtaja kigogo huyo) anapata wapi viwanja? Uongo huo wa kijinga. Mimi nilienda pale kushiriki maandamano kwa sababu ni mdau, si vinginevyo.

“Hebu fikiria, hivi unaona tofauti za bei za bia? Bia za nje na ndani ziko sawasawa? Zinatofautiana kwa sababu ya kodi na ili kulinda viwanda vya ndani,” alisema muigizaji huyo maarufu.

Kwa upande wa Rich, naye kama walivyo wenzake, alisema madai ya kupewa hongo ya viwanja na fedha ni ya uongo, kwani yeye alianza kushiriki kampeni za kukamata filamu za nje tangu enzi zile Nape Nnauye akiwa Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo.

“Kwanza mimi siyo timu (kigogo), nilienda pale kama mdau na wala sikwenda pale kupinga kazi za nje, nilienda pale kutaka filamu zote zilipe kodi. Tatizo la filamu zetu siyo zile za nje, bali ni ubovu wa kazi zetu.

“Kama tutatengeneza kazi nzuri zitauzika tu sokoni, lakini kama kila mtu mwenye fedha anadhani anaweza kutengeneza filamu, hiyo ndiyo inayoharibu soko letu. Ninakubali kuna udhaifu katika filamu za ndani, ambazo nadhani ndiyo zinachangia kuua soko, si filamu za nje,” alisema.

Leave A Reply