The House of Favourite Newspapers

Jembe jipya lashtua Yanga

0

UWEZO uliooneshwa na jembe jipya la Yanga kutokea Ghana katika mchezo wa kirafiki dhidi ya JKU uliochezwa juzi Jumapili, umewashtua wengi.

Mghana huyo aliyewahi kucheza Medeama ya nchini humo, aitwaye Godfred Nyarko, tayari ameonekana kumvutia Kocha Mkuu wa Yanga, Nasreddine Nabi ambaye amesema kama ataendelea kufanya vizuri, basi atasajiliwa kwenye dirisha dogo msimu huu.

Akizungumza kuhusu kiungo huyo, Kocha Nabi alisema: “Ni kweli tuna mchezaji mpya kwenye kikosi chetu, ni mchezaji ambaye yupo kwa majaribio.

“Kama kila kitu kitaenda vizuri na akafuzu majaribio yake basi tutafanya mpango wa kumuongeza katika kipindi cha dirisha dogo ili kukiongezea nguvu kikosi chetu katika vita ya ubingwa msimu huu.”

Kwa upande wa Mwenyekiti wa Kamati ya Ufundi Yanga, Dominick Albinus, aliliambia Spoti Xtra kwamba: “Ni kweli kuna ingizo la mchezaji kwenye kikosi chetu lakini yuko pale kwa ajili ya kufanya majaribio, ni Mghana ila sikumbuki ametoka timu gani lakini kwa sasa ni mchezaji huru.

“Ana mwezi mmoja na Kocha Nabi ameomba aendelee kufanya majaribio kwa ajili ya kujiridhisha ili kwenye dirisha dogo la usajili aweze kumsajili kama atamshawishi. Ataendelea kuwepo Yanga kwenye mazoezi pamoja na mechi za kirafiki.”

Kiungo huyo mwenye miaka 23, timu yake ya mwisho kuitumikia ni Medeama SC ya Ghana kabla ya kuwa mchezaji huru.

~~ JOEL THOMAS NA LEEN ESSAU

Leave A Reply