Jembe Jipya Yanga SC Laanza na Sakho
BEKI mpya wa kushoto wa Yanga, David Bryson, ameanza na bahati baada ya kutupia bao moja katika ushindi wa 3-1 dhidi ya DTB kwenye mchezo wa kirafiki.
Bao hilo alilolifunga huenda likawa kama salamu kwa watani wao wa jadi, Simba ambao leo Jumamosi watavaana katika mchezo wa Ngao ya Jamii utakaochezwa Uwanja wa Mkapa, Dar.
Beki huyo aliyerejea uwanjani hivi karibuni akitokea katika majeraha ya misuli, huenda akawa sehemu ya kikosi kitakachocheza dhidi ya Simba, huku akitarajiwa kukabana na Ousmane Sakho.
Wakati Bryson akifunga bao hilo, straika, Fiston Mayele ameendelea kuonesha makali yake kwa kucheka na nyavu ambapo alifunga moja.
Akizungumza na Spoti Xtra, Mkuu wa Kitengo cha Habari na Mawasiliano wa Yanga, Hassani Bumbuli, alisema mchezo huo ulikuwa maalum kwa Kocha Nasreddine Nabi kuwajaribu nyota wake ambao hawakupata nafasi katika michezo iliyopita, huku akiwataja wafungaji kuwa ni Mayele, Bryson na Yusuf Athuman.
WILBERT MOLANDI, Dar es Salaam