The House of Favourite Newspapers

JINSI YA KUJIKINGA NA MAUMIVU WAKATI WA HEDHI (DYSMENORRHEA)

WANAWAKE wengi wamekuwa wakisumbuliwa na tatizo la kupata maumivu wakati wa hedhi ambalo kitaalam huitwa period pains.  Period pains ni maumivu yanayotokea sehemu ya chini ya tumbo au kiuno wakati mwanamke anapoanza kuingia kwenye siku zake.

Maumivu haya huanza pale mayai yanapotoka katika mirija yaani fallopian tubes na kuteremka chini ya mirija hiyo wakati wa urutubishwaji wa mayai, yaani ovulation. Maumivu haya huweza kuwa makali au ya kawaida hivyo kuna aina mbili za maumivu wakati wa hedhi; Aina hizo ni;

  1. A) PRIMARY DYSMENORRHEA (MENARCHEA)

Haya ni maumivu yasiyokuwa na sababu maalum. Katika aina hii, maumivu ni ya kawaida na hutokea sehemu ya chini ya tumbo na kiunoni. Pia maumivu haya huanza siku moja au mbili kabla ya hedhi na kumalizika baada ya siku tatu au ya nne kulingana na mwili wa mtu husika.

Maumivu haya hutokana na uongezekaji wa tindikali kitaalam huitwa prostaglinds ambayo hutokea siku chache baada ya yai kupevuka na kufanya misuli kusinyaa hivyo kusinyaa huko husababisha tumbo kupata maumivu wakati wa hedhi.

  1. B) SECONDARY DYSMENORRHEA

Haya ni maumivu yanayotokea kutokana na sababu mbalimbali kama vile matatizo katika kizazi, ugonjwa wa nyonga na matatizo katika mirija ya mayai ya mwanamke. Asilimia 60 ya wanawake au wasichana wanasumbuliwa na tatizo hili la kupata maumivu wakati wa hedhi. Pia baadhi ya wanawake au wasichana hupata maumivu haya zaidi na kusababisha kulazwa au kushindwa kufanya kazi zao za kila siku.

Pia huweza kusababishwa na viuvimbe vidogodogo katika via vya uzazi yaani fibroids. Maambukizi sugu katika via vya uzazi -PID Endometriosis, Ovarian Cyst na viwambo vya mpango wa uzazi vinavyoingizwa katika kizazi, kwa mfano vitanzi, vijiti, vidonge vya kuzuia mimba (ambavyo huwa na progesterone ambayo pia huweza kusababisha ugonjwa wa moyo.)

DALILI ZA DYSMENORRHEA

Dalili za ugonjwa huu kwa wanawake na wasichana ni kuwa na maumivu makali wakati wa hedhi. Kupata kichefuchefu, kutapika wakati wa hedhi, kuharisha wakati wa hedhi, kupata maumivu chini ya kitovu, maumivu ya mgongo na maumivu ya kiuno wakati wa hedhi.

MATIBABU

Zipo njia nyingi za kutibia maumivu ya hedhi baada ya kuonwa na daktari. Mojawapo ni kuweka chupa au mfuko wenye maji ya moto kwenye sehemu ya chini ya tumbo. Hii ni njia inayotumika kama njia ya dharura, lakini hakikisha mfuko huo usiwe wa moto mkali wa kuunguza ngozi. Daktari akimuona mgonjwa anaweza kumpa dawa za kutuliza maumivu kama ibuprofen, mefenamic acid na proxen.

Matumizi ya vidonge vya uzazi wa mpango pia husaidia kupunguza maumivu ya hedhi. Kama ilivyo kwa dawa nyingine, ni muhimu kupata ushauri wa kitaalam kabla ya kuanza kutumia dawa hizi. Iwapo njia hizi hazifanikiwi kutuliza maumivu ya hedhi, vipimo zaidi vinahitajika ili kugundua chanzo cha maumivu hayo ili kitibiwe.

Miongoni mwa vipimo vinavyohitajika ni vipimo vya magonjwa ya maambukizi (infection) ya njia ya uzazi pamoja na upasuaji ili kuona kama kuna uwepo wa endometriosis na kuiondoa. Zipo tiba kwa njia ya upasuaji unaofanyika kwa kutumia matundu madogo na kamera bila kufungua tumbo.

Iwapo maumivu ni makali sana na hayatibiki kwa dawa, mgonjwa asiyekuwa na mpango wa kupata mtoto hushauriwa kuondoa kifuko cha uzazi ili kuepuka kifo.

JINSI YA KUJIKINGA NA KUMALIZA TATIZO HILI

Usiwe mtu mwenye mawazo, ondoa hali ya mfadhaiko, punguza ulaji wa vyakula vyenye mafuta na sodium kama vile chipsi, vyakula vya kusindikwa kwenye makopo (canned foods), vyakula vyenye chumvi nyingi na kadhalika.

Pia punguza vinywaji vyenye caffeine kama kahawa au vinywaji vyote vyenye vilevi na chai yenye viungo vingi ila unaweza kunywa angalau kikombe kimoja cha chai na si zaidi ya hapo kwa siku moja pia zingatia lishe bora ya vyakula na kula matunda kwa wingi.

Vilevile kunywa maji mengi angalau lita tatu kwa siku. Fanya mazoezi mara kwa mara. Kwa ushauri zaidi wasiliana nami kwa simu hiyo hapo.

Comments are closed.