The House of Favourite Newspapers

JOHN BOCCO: BADO TU NA NAFASI, SUBIRINI MUONE

NAHODHA na Mshambuliaji tegemeo wa Simba, John Bocco, amesema bado wana nafasi ya kufuzu hatua inayofuata ya Ligi ya Mabingwa Afrika.

 

Bocco alitoa kauli hiyo muda mfupi baada ya Simba kupokea kichapo cha mabao 2-0 ugenini dhidi ya JS Saoura ya Algeria na kutumbukia mkiani mwa Kundi D.

 

Simba baada ya matokeo hayo, wamejikuta wapo mkiani kwenye kundi D, Saoura akiongoza akiwa na pointi 8, Al Ahly 7, AS Vita 7 na Simba wenyewe 6 huku kila timu ikiwa imebakisha mchezo mmoja, na ikiwa na nafasi ya kufuzu.

 

Akizungumza na Championi Jumatatu, Bocco alisema kuwa matokeo hayo waliyoyapata yasiwaogopeshe mashabiki wa Simba, kwani wana matumaini makubwa ya kushinda mchezo wa nyumbani dhidi ya AS Vita.

 

Bocco alisema, anaamini kocha wao Mbelgiji, Patrick Aussems, ameona upungufu wa timu yao katika mchezo huo dhidi ya Saoura uliosababisha wapoteze ugenini, hivyo atafanyia marekebisho kuhakikisha mchezo ujao na AS Vita wanapata ushindi.

 

“Tunafahamu Mashabiki wetu wameumia baada ya matokeo ya mchezo wetu na Saoura, sisi pia tumeumia kama wachezaji, kwani ni matokeo ambayo hatukuyatarajia.

 

“Sisi tuliingia uwanjani kwa lengo moja la kushinda mchezo huu, lakini kama mnavyofahamu soka lina matokeo matatu; kushinda, kufungwa au sare.

 

“Kikubwa tunajipanga kwa ajili ya mchezo ujao na Vita, katika mchezo huu tunahitaji ushindi wa aina yoyote ili kuhakikisha tunafuzu hatua inayofuata na hilo linawezekana kwetu, kwani tutakuwa nyumbani, hivyo sapoti ya mashabiki itatusaidia kutuongezea morali ndani ya uwanja,” alisema Bocco.

WILBERT MOLANDI, Dar es Salaam

Comments are closed.