The House of Favourite Newspapers

JOKATE YAMKUTA YA AMINA CHIFUPA

SIKU tatu baada ya Mwanamitindo Jokate Mwegelo kuteuliwa kuwa Mkuu wa Wilaya ya Kisarawe mkoani Pwani, gumzo la aina yake limeibuka kumhusu mrembo huyo kitendo ambacho kimeshabihiana na mambo yaliyomtokea marehemu Amina Chifupa aliyekuwa mbunge wa kuteuliwa. Jokate aliteuliwa Julai 28, mwa­ka huu baada ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Magufuli kufanya mabadiliko ya wizara, mikoa na wilaya.

MITANDAO YAANZA KUMUANDAMA

Mara baada kuteuliwa, mijadala mbalimbali iliibuka mitandaoni kwa watu kuonesha kumkubali lakini wengine wakione­sha kutomkubali kutokana na nafasi yake aliyokuwa nayo awali ya uanamitin­do. Waliokuwa wanamku­bali, walijenga hoja kuwa mrembo huyo ana ujasiri, ana hekima na anaweza kumsaidia rais katika nafa­si hiyo ya ukuu wa wilaya kwani kupitia taasisi yake ya Kidoti, ameshafanya mambo makubwa kwenye jamii.

“Huyu Jokate mna­muona hivi tu lakini mimi nawaambia ni mtu ambaye anajua kusimamia vitu, ana hekima na busara hivyo jukumu la ukuu wa wilaya naamini kabisa ana­kwenda kulitendea haki. “Unajua hata mheshimiwa mwenyewe hadi kufikia hatua ya kumteua, ameona mbali kwa mrembo huyu hivyo kamwe hawezi kumuangusha,” alichangia mdau aliyejitambulisha kwa jina la Ibra katika mtandao wa Instagram.Picha inayohusiana

HOJA YA WALIOMKOSOA

Waliokosoa wengi wao walisimamia hoja ya up­ole wa Jokate na kudai kwamba pengine anaweza kushindwa kuwakemea watumishi ambao watakuwa chini yake. “Unajua kasi ya JPM bwana sasa hivi ni mwendo wa maagizo na kusimamia mambo yaende kwa haraka sasa nikimtazama Jokate namuona kama mpole hivi,” alichangia mdau mmoja mtandaoni aliyejiita Kije.

MJADALA WAZIDI  KUTAWALA

Mwanamitindo huyo alizidi kujadiliwa na kutazamwa zaidi katika mtandao wa YouTube ambapo kwenye kila video ya uteuzi wake iliyowekwa na akaunti mbalimbali za mtandao huo, ilionekana kutazamwa na watu wengi zaidi kuliko wa­teule wengine walioteuliwa na rais siku hiyo.

Mbali na kutazamwa, watu ‘walikomenti’ maoni mbalimbali kwa kila mmoja kuweka maoni na mtazamo wake juu ya Jokate huku wengine wakikumbushia safari yake ya kisanii na hata kisisiasa akiwa Umoja wa Vijana Kitengo cha Chipukizi katika Chama Cha Mapin­duzi (CCM).

Kuhusu wale waliomp­inga, mchambuzi mmoja wa masuala ya masuala ya kisiasa aliyeongea na Uwazi, alisema kinachomtokea Jokate ni sawa na kilichom­tokea marehemu Amina Chifupa lakini anaamini atakuja kufanya vizuri na kuwashangaza Watanzania.

“Unajua Amina alipo­teuliwa mwaka 2005 kuwa Mbunge wa Viti Maalum mkoa wa Dar es Salaam akitokea kwenye utangazaji akiwa mrembo watu wal­iona labda pengine Umoja wa Vijana (CCM) walikosea kufanya uteuzi huo bila kujua kwamba waliona kitu kwake na baadaye akaja kuwashangaza.

“Walianza kumsema sana, wakamponda wee, wakam­zushia mambo kibao lakini mwisho wa siku mambo yakaja kuwa tofauti. Amina alikuja kuonesha makucha yake baadaye kwamba ni jasiri, mchapakazi na mtu ambaye aliibua na kukemea suala zima la madawa ya kulevya ambalo lilikuwa ni tatizo kubwa nchini ambalo lilihusisha baadhi ya vigogo serikalini,” alisema mcham­buzi huyo na kuongeza:

“Mimi nafikiri tumpe muda tu Jokate, mimi naamini kabisa huyu binti atafanya mambo makubwa sana ka­tika nafasi yake na ninamta­biria anaweza kufika mbali sana kisiasa endapo atazidi kujipambanua katika siasa kwani nguvu ya ushawishi anayo.”Tokeo la picha la amina chifupa

NGAWAIYA AMPA TANO

Naye mbunge wa zamani wa Moshi Vijijini, Thomas Ngawaiya akizungumzia uteuzi huo, alisema rais anachagua vijana zaidi katika nafasi mbalimbali kutokana na kuwa na nguvu ya kufanya kazi kwa masaa mengi bila kuchoka na wengi wao wana elimu ya juu hivyo kutomuangusha. “Rais ana imani kubwa na vijana sababu anaamini wanaweza kufanya kazi kwa saa nyingi na pia wengi hawajamuangusha hivyo amezidi kuwapa nafasi na mimi naona ni jambo jema,” alisema Ngawaiya.

UTEUZI WA JERRY MURO NAO WAIBUA MANENO

Mbali na Jokate, uteuzi wa aliyewahi kuwa msemaji wa Timu ya Yanga, Jerry Muro ambaye amekuwa Mkuu wa Wilaya ya Arumeru, nao uliibua maneno huku wengi wakidai kuwa huenda mwa­nahabari huyo akawa na yale maneno ya ‘shombo’ ya kimpira katika nafasi hiyo.

Lakini hata hivyo, wen­gine waliochangia kwenye mitandao ya kijamii wal­isema Jerry anaweza ku­fanya vizuri katika nafasi hiyo kwani safari yake ya uana­habari na kisiasa, imeonesha ni mzalendo wa kweli na mtu mwenye kupenda haki itendeke.Tokeo la picha la JOKATE

Wengi waliochangia hoja hiyo walishibisha zaidi kwa kukumbushia sakata la rushwa kwa madereva na askari wa usalama barabara­ni alilofichua mwaka 2010 akiwa mwanahabari. Walisema ni mtu ambaye aliichukia rushwa, jasiri, ali­jitoa muhanga kuhakikisha anakomesha tatizo hilo na kweli matunda yalionekana kwa kurusha picha za ma­dereva wakitoa rushwa na kupokelewa na askari wa usalama barabarani.

Akizungumza na mwa­nahabari wetu siku moja kabla ya kuteuliwa kushika wadhifa huo, Jerry alisema amekuwa akiwasaidia sana wananchi wa kijijini kwake Machame, Moshi. “Kwa kweli nimekuwa pamoja na wananchi wa kiji­jini kwangu, nafarijika kuona nawasaidia kwa hali na mali, na ndio maana ng’ombe wangu wakizaa huwa natoa ndama kwenye vikundi vya akina mama,” alisema Jerry.

Stori: MWANDISHI WETU, Dar

Comments are closed.