The House of Favourite Newspapers

JPM AWASHTUKIZA MAGEREZA UKONGA, AFANYA MAAMUZI MAGUMU – VIDEO

Rais Magufuli afanya ziara ya kushtukiza katika mradi wa ujenzi wa nyumba za makazi ya Askari Magereza wa gereza la Ukonga Dar es Salaam, asema hajaridhishwa na utendaji kazi wa TBA, aagiza mradi huo ukabidhiwe JWTZ

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli tarehe 16 Machi, 2019 amefanya ziara ya kushtukiza katika mradi wa ujenzi wa nyumba za makazi ya Askari Magereza wa gereza la Ukonga Jijini Dar es Salaam na kuagiza mradi huo ukabidhiwe kwa Jeshi la Ulinzi la Wananchi Tanzania (JWTZ).

Mhe. Rais Magufuli ametoa maagizo hayo baada ya kubaini kuwa Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) imeshindwa kutekeleza mradi huo kwa wakati, licha ya Serikali kutoa shilingi Bilioni 10 za ujenzi.

Rais Magufuli akimwangalia Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Magereza Julius Ntembala akipima nguzo wakati akikagua maendeleo ya ujenzi wa nyumba za askari Magereza, Ukonga jijini Dar es salaam alipofanya ziara ya kushtukiza leo Jumamosi Machi 16, 2019

Ametaka wataalamu wa TBA waliokuwa wakisimamia mradi huo pamoja na Askari Magereza waondoke na kuwapisha JWTZ.

“Kwa hiyo hapa nisimuone mtu wa TBA, nisimuone mtu wa Magereza kuja kusimamia, muwaache Jeshi la Wananchi wafanye kazi zao, siku watakapokuja kunikabidhi na mimi nitawakabidhi Magereza, kwa hiyo watu wa TBA kuanzia leo nimewafukuza hapa” amesema Mhe. Rais Magufuli.

Mhe. Rais Magufuli ameelezea kutoridhishwa na utendaji kazi wa TBA katika mradio huo ambao ulianza zaidi ya miaka 2 iliyopita kwa kushirikisha Jeshi la Magereza ambalo lilikuwa linaisadia TBA katika kazi za ujenzi, na ametaka TBA na Jeshi la Magereza wabadilike katika utekelezaji wa majukumu yao.

Rais Magufuli akiangalia jiwe la msingi la ujenzi wa nyumba za ghorofa za Magomeni Kota jijini Dar es salaam alizoziwekea mnamo Aprili 15, 2017 ambapo mpaka sasa ujenzi wake umesimama.

“Nataka kila mlipo watu wa Magereza mfanye kazi, msimamie watu, kama ni ng’ombe muwafuge vizuri wazalishe vizuri hadi muuze mazao nje, kama ni kilimo mlime kwelikweli, muwe ni jeshi la kuzalisha, hii ni aibu kuleta jeshi jingine la wananchi kuja kuwajengea nyumba nyinyi, wakati nyumba mnakaa nyinyi, mlitakiwa muwe mmeshapanga mkakati kwamba TBA wamesuasua, ngoja tufyatue matofari, tuanze kujenga” amesisitiza Mhe. Rais Magufuli.

Mkuu wa Utawala wa Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) Kanali Charles Mbuge amesema JKT itakamilisha ujenzi huo ndani ya kipindi cha miezi 2 na nusu kuanzia kesho na kwamba kazi zitafanywa usiku na mchana.

Aidha, Mhe. Rais Magufuli ameitaka TBA kutoa maelezo ya namna fedha zilizotolewa na Serikali kiasi cha shilingi Bilioni 10 zilivyotumika, na ameonya kuwa endapo itabainika matumizi ya fedha hizo hayaendani na kazi zilizofanyika hatua kali zitachukuliwa.

Katika mradi huo, ujenzi wa majengo 12 ya makazi ya Askari Magereza yaliyopangwa kuwa na ghorofa 4 kila moja ulioanza Desemba 2016 umefikia asilimia 45 tu na unaendelea kwa kusuasua.

Wakati huo huo, Mhe. Rais Magufuli amefanya ziara ya kushtukiza katika mradi wa ujenzi wa majengo ya makazi wa Magomeni Kota Jijini Dar es Salaam na kuelezea kusikitishwa na hali ya kusuasua kwa ujenzi huo ulioanza Aprili 2017.

Mhe. Rais Magufuli ameshuhudia ujenzi wa majengo yenye ghorofa 3 ukiwa umefikia asilimia 36 na kazi za ujenzi zikiwa zimesimama kwa muda usiojulikana.

Mmoja wa wananchi wanaosubiri kukamilika kwa ujenzi wa nyumba hizo Mzee Omary Mpimbila amemueleza Mhe. Rais Magufuli kuwa wamekuwa wakifanya juhudi za kufuatilia hatma ya majengo hayo kutoka TBA na Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano lakini mpaka sasa hawajapatiwa majibu ya sababu za kutelekezwa kwake.

Mhe. Rais Magufuli ameahidi kuchukua hatua za haraka kuhakikisha ujenzi huo unaendelea na wakazi wa Magomeni Kota wanapatiwa makazi kama walivyoahidiwa.

Gerson Msigwa
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU
Dar es Salaam
16 Machi, 2019

JPM AWASIMAMISHA TBA UJENZI NYUMBA ZA MAGEREZA

Comments are closed.