JPM Azindua Hifadhi ya Taifa Burigi, Ampongeza Faru Rajabu – Video
Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli, amempongeza faru Rajabu, ambaye ni mtoto wa Faru John, kwa juhudi zake za uzalishaji na kuzidi kuongeza idadi ya faru hadi kufikia faru140, katika hifadhi ya Taifa ya Serengeti.
Rais Magufuli ameyabainisha hayo leo Julai 9, wakati wa Uzinduzi wa Hifadhi ya Taifa ya Burigi, iliyopatikana mara baada ya mapori matatu ya akiba kuunganishwa, likiwemo pori la Burigi, Biharamulo na Kimisi Wilayani Chato Mkoani Geita.
“Wanahabari wa Azamt Tv ilikua tushiriki nao leo katika shughuli ya leo lakini kwa bahati mbaya jana wakiwa katika Mkoa wa Singida walitangulia mbele ya haki , tumuombe Mwenyezi Mungu azitunze roho zao na majeruhi waweze kupona mapema.
“Naipongeza Wizara na wadau wa utalii, kwa kuiwezesha hifadhi ya Serengeti kushinda tuzo, wapo watu wamezoea kusema mabaya tu mazuri hawayasemi, yapo tunayoshindwa lakini haya ya uhifadhi tunashinda, mpira tunapigwa na sisi kwenye uhifadhi tunawapiga.
“Wapo wanaotutuhumu kuwa hatupendi mazingira, hili si kweli hata kidogo, tungekuwa hatupendi mazingira tusingetenga maeneo makubwa ya uhifadhi na kuanzisha hifadhi kama hizi tatu.
“Idadi ya tembo imeongezeka kutoka 43,330 mwaka 2016 hadi kufikia zaidi ya 60,000. Faru wameongezeka kufikia 163 hivyo hatuna budi kumpongeza Faru Rajabu (mtoto wa faru John) ambae ameshazalisha watoto 40. Nadhani yule wa jina wangu alikuwa hajitumi vizuri.
“Nawaambia zaeni tu,ukishakuwa na idadi kubwa umetengeneza uchumi ndio maana uchumi wa China upo juu kutokana na population, najua nikizungumza hili wale watu ambao wamezoea kubania mayai watalalamika sana, nyinyi yaachieni waacheni wayabanie ya kwao
“Ninatoa wito kwa Wizara ya Maliasili na Utalii kuendelea kujipanga na kuweka mikakati ya kuongeza watalii nchini, miongoni mwa malalamiko ambayo nimekuwa nikiyapata ni pamoja na gharama za utalii kuwa juu na malalamiko mengine,” amesema Rais Magufuli.
Comments are closed.