The House of Favourite Newspapers

Kagere Aifanyia Yanga Kitu Mbaya

0

LICHA ya Ligi Kuu Bara kusimama kwa muda kutokana na ugonjwa wa Corona, mshambuliaji wa Simba, Mnyarwanda, Meddie Kagere, amefanikiwa kuandika rekodi nyingine ya kibabe akiwa na kikosi cha timu hiyo ukilinganisha na msimu uliopita wakati alipokuwa akishirikiana na Mganda, Emmanuel Okwi katika safu ya ushambuliaji ya timu hiyo.

 

Rekodi hiyo si nyingine bali ni ile ya kuiongoza timu hiyo kuvunja baadhi ya rekodi za wapinzani wao wa jadi, Yanga za msimu uliopita mapema kabisa kabla ya ligi kuu kufikia tamati.

 

Mpaka kufikia sasa, Simba ambayo inaongoza msimamo wa ligi kuu ikiwa na pointi 71, tayari imevunja rekodi ya mabao ambayo Yanga iliyafunga katika mechi zake zote za ligi kuu ilizocheza msimu uliopita na hivi sasa inapambana kuhakikisha inaifikia rekodi nyingine ya Yanga waliyoiweka msimu wa 2015/16.

 

Msimu uliopita, Yanga ilifanikiwa kumaliza ligi hiyo ikiwa imefunga mabao 56, ambayo kwa sasa tayari Simba imeishayavuka. Mpaka sasa Simba imeshafunga mabao ya 63 huku Kagere peke yake katika mabao hayo, akiwa amefunga mabao 19.

 

Hata hivyo, wakati michuano hiyo itakaporejea, baada ya kumalizika kwa zuio la serikali la kufanya mikusanyiko kutokana na ugonjwa wa Corona, Kagere atakuwa na jukumu jingine la kuiongoza timu hiyo kuhakikisha inafikisha idadi ya mabao ambayo Yanga ilifunga msimu wa 2015/16 ilipofunga mabao 70, lakini pia wakati huo akitakiwa kuiongoza timu hiyo kuvunja rekodi yake ya msimu uliopita, ya mabao 77.

SWEETBERT LUKONGE, Dar es Salaam

Leave A Reply