The House of Favourite Newspapers

Kagere Ampa Akili Bocco, Ajiongezea Dozi

John Bocco

UJIO wa straika Mnyarwanda, Meddie Kagere Simba umemfanya nahodha na mshambuliaji wa Simba, John Bocco aongeze dozi ya mazoezi ambayo alikuwa anafanya kila siku kwa ajili ya kuwa fiti kwa ajili ya vita ya kupambania nafasi ya kuanza.

 

Bocco ambaye aliiongoza timu hiyo kutwaa ubingwa wa ligi kuu msimu uliopita ni miongoni mwa nyota ambao wapo katika kambi nchini Uturuki kwa ajili ya kujiandaa na msimu ujao wa Ligi Kuu Bara ambayo imepangwa kuanza Agosti 22, Simba wakianza na Tanzania Prisons katika Uwanja wa Taifa jijini Dar.

Meddie Kagere

Simba imewasajili Kagere, Adam Salamba, Mohamed Rashid, Hassan Dilunga na Marcel Kaheza katika kuiboresha safu yake ya ushambuliaji.

 

Bocco ameliambia Spoti Xtra, kuwa kwake ujio wa nyota huyo utaongeza ushindani kwa timu yao lakini utaongeza juhudi ya mazoezi kwa wachezaji kwa nia ya kutaka kila mmoja awe fiti ili acheze timu ya kwanza.

 

“Ukiwa kama mchezaji na ukaogopa changamoto basi hufai kuitwa mchezaji ninaamini uwepo wa wachezaji wapya utaongeza kitu miongoni mwetu.”

 

“Sasa kila mtu atajituma zaidi yaani kama alikuwa anafanya mara mbili basi baada ya mazoezi atafanya mara tatu au nne ili tu awe fiti zaidi na apate namba jambo ambalo litakuwa na faida kubwa kwetu na kwa timu nzima.

 

“Mchezaji ambaye atapata nafasi atafanya kwa juhudi kubwa ili aonyeshe kwa benchi la ufundi kwamba hawakukosea kumpa nafasi, kwangu hilo ni jambo bora na lina manufaa kwa timu kwa msimu ujao,” alisema Bocco ambaye ni miongoni mwa wachezaji wachache wazawa wanaojielewa nchini.

Comments are closed.