Kagere Aweka Rekodi ya Kibabe Bongo
MSHAMBULIAJIwa kimataifa wa Simba, Mnyarwanda, Meddie Kagere, ameandika rekodi mpya na ya kibabe ndani ya Ligi Kuu Bara baada ya juzi kufunga bao lake la 50 kwenye ligi tangu alipoanza rasmi kuichezea Simba.
Kagere ameandika rekodi hiyo juzi usiku baada ya kufunga bao la mkwaju wa penalti dakika ya 75 ya mchezo dhidi ya KMC ulioisha kwa Simba kuibuka na ushindi wa bao 1-0.
Huu ni msimu wa tatu, kwa Kagere ndani ya kikosi cha Simba aliyojiunga nayo rasmi Juni 27, mwaka 2018 akitokea Gor Mahia ya Kenya.
Kagere amefunga mabao hayo ndani ya misimu mitatu, akianza msimu wa 2018/19 ambao alifunga 23 kabla ya msimu uliopita wa 2019/20 kuweka kambani mabao 22, huku msimu huu akiwa ameweka kambani mabao matano mpaka sasa.
Akizungumza baada ya kuweka rekodi hiyo, Kagere alisema: “Safari bado inaendelea.
Shukurani kwa yeyote ambaye alikuwa sehemu ya mafanikio haya, kwa Mwenyezi Mungu kila kitu kinawezekana.”Ikumbukwe pia kuwa Kagere ndiye anakamatia Tuzo ya Mfungaji Bora kwa misimu miwili mfululizo.
Stori: Joel Thomas,Dar es Salaam