The House of Favourite Newspapers

Kagere, Bocco Wakabidhiwa Ushindi wa Simba SC

WACHEZAJI wa Simba wakiongozwa na washambuliaji, Meddie Kagere na John Bocco wamepewa jukumu zito la kuhakikisha wanaivusha timu hiyo katika hatua ya nusu fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika.

 

Simba inatarajia kutupa karata yake ya kwanza ya Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya UD do Songo ya Msumbiji katika mchezo wa awali kwa kuanzia ugenini wikiendi hii.

Msimu uliopita, Simba ilifanikiwa kufika hatua ya Robo Fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika na kutolewa katika hatua hiyo, hivyo kusababisha kuiletea neema nchi kwa timu nne za Tanzania kushiriki mashindano ya kimataifa.

 

Akizungumza na Championi Jumatano, Mtendaji Mkuu wa Simba, Crescentius Magori amesema kuwa, wamejiandaa ipasavyo kuhakikisha msimu huu wanafanikiwa kufika hatua ya nusu fainali au fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika na ndiyo maana wamefanya usajili makini.

“Tunahitaji Simba ya kisasa kuelekea msimu ujao wa ligi kuu na mashindano ya kimataifa na ndio maana tumefanya usajili makini ambao utatusaidia kufika mbali zaidi, tunachohitaji ni kuona tunafika hatua ya nusu fainali au fainali ya Ligi ya Mabingwa.

 

“Kikosi chetu kipo vizuri, kambi ambayo timu iliweka Afrika Kusini imeweza kuwasaidia wachezaji katika kujiimarisha kwenye ligi na mashindano ya kimataifa,” alisema Magori.

Comments are closed.