The House of Favourite Newspapers

Kagere, Bocco wapewa milioni 50

MNYARWANDA, Meddie Kagere na John Bocco, ni miongoni mwa wachezaji wa Simba watakaogawana kitita kinono cha shilingi milioni 50 kilichotolewa na uongozi wa klabu hiyo baada ya kuifunga Yanga juzi Jumamosi katika mchezo wa Ligi Kuu Bara Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

 

Kagere na Bocco juzi walifanya kazi nzuri, Bocco akitoa asisti na Kagere akifunga bao muhimu lililosababisha ushindi huo. Sasa taarifa ni kwamba ushindi huo umewapa Sh milioni 50 wachezaji wa Simba. Hiyo ni motisha baada ya kuwagaragaza watani wao wa jadi.

 

Fedha hizo watapewa kutoka kwa uongozi makini wa Simba chini ya mwekezaji bilionea kijana Afrika, Mohammed Dewji ‘Mo’.

Habari za kuaminika kutoka ndani ya timu hiyo ambazo Championi Jumatatu limezipata zimedai kabla ya mechi hiyo, Mo aliwaahidi wachezaji hao kuwapatia kitita cha Sh milioni 50 wagawane kama wataifunga Yanga.

 

Kwa hiyo, kutokana na ushindi huo wa bao 1-0 lililofungwa na Kagere walioupata hiyo juzi dhidi ya Yanga wachezaji hao wamefanikiwa kuchukua kitita hicho cha Sh 50 milioni kutoka kwa bilionea huyo.

“Fedha hizo bado hatujapewa lakini muda wowote tunaweza kuingiziwa kwenye akaunti yetu kama ambavyo hufanyika siku zote.

 

“Hata hivyo mpaka sasa bado sijajua mgawo utakuwaje kwa waliocheza na wale ambao hawajacheza lakini waliocheza watachukua nyingi, wanawaza kuondoka na milioni mbili na kiasi kitakachobakia kitagawanywa kwa wale ambao hawajacheza,” kilisema chanzo hicho cha habari.

Awali, kulikuwa na tetesi kwamba kila mchezaji angepewa Sh milioni 4 lakini sasa imebainika rasmi kuwa watagawana milioni 50.

 

Mratibu wa timu hiyo, Abbas Ally, alipoulizwa kuhusiana na hilo, alisema kuwa utaratibu wa uongozi wa timu hiyo kutoa motisha kwa wachezaji wao pindi wanapofanya vizuri uwanjani ni wa siku zote, kwa hiyo, kuna fedha watapata baada ya kushinda mechi hiyo.

 

SWEETBERTLUKONGE, Dar es Salaam

Comments are closed.