The House of Favourite Newspapers

Kaizer Chiefs Watua Kwa Lokosa wa Simba

0

MIAMBA ya soka kutokea nchini Afrika Kusini, Kaizer Chiefs wameonyesha nia ya kumsajili mshambuliaji wa Klabu ya Simba raia wa Nigeria, Junior Lokosa, ambapo inaelezwa Simba wanahitaji dau la dola 200,000 sawa na zaidi ya Shilingi Milioni 464.

 

Lokosa ambaye alijiunga na Simba kwenye dirisha la usajili la mwezi Januari, tangu ajiunge na kikosi cha timu hiyo ameonekana kupata wakati mgumu kuingia kwenye kikosi cha kwanza cha Simba, mbele ya Chris Mugalu ambaye ameonekana kuwa chaguo la kwanza la Kocha Didier Gomes.

 

Tangu ajiunge na Simba Januari mwaka huu kwa ajili ya kutumika kwenye michuano ya kimataifa akisaini mkataba wa miezi sita ambao una kipengele cha kumuongeza mwingine ikiwa atafanya vizuri, Lokosa ameichezea Simba kwa dakika 15 tu kwenye mchezo mmoja wa Simba Super Cup ambapo alicheza dhidi ya TP Mazembe, Januari 31, mwaka huu.

 

Inaelezwa pia kuwa kikosi cha Strømsgodset Toppfotball ya nchini Norway, kilichoonyesha nia ya kumuhitaji nyota huyo kimejiondoa kwenye mpango huo.

Chanzo cha kuaminika kutoka ndani ya kikosi cha Klabu ya Simba kimelitonya Championi Jumamosi, kuwa zipo klabu ambazo zimeonyesha nia ya kumuhitaji Lokosa ikiwemo Kaizer Chiefs, ambapo Simba imeweka wazi kwamba thamani ya nyota huyo ni kiasi cha dola 200,000.

 

Inadaiwa Simba watakuwa tayari kumuachia Lokosa ambaye ameshindwa kupata nafasi kwenye kikosi cha Gomes ambaye naye ameonekana kutokuwa na mpango naye kutokana na kutokuwa fiti.

 

Akizungumzia ofa hiyo ya Kaizer Chief, Katibu Mkuu wa Simba, Dk Arnold Kashembe ameliambia Championi Jumamosi: “Sijapokea taarifa zozote kuhusiana na ofa ya Klabu ya Kaizer Chief kumtaka mshambuliaji wetu, Junior Lokosa.

 

“Hivyo siwezi kusema lolote kwa sasa lakini iwapo kutakuwa na taarifa yoyote rasmi kuhusiana na hilo basi tutawaeleza.”

Stori: Said Ally na Joel Thomas | Championi Ijumaa

Leave A Reply