The House of Favourite Newspapers

Kakolanya, Manula Wampasua Kichwa Mbelgiji Simba

KOCHA Mkuu wa Simba, Mbelgiji, Patrick Aussems, amekiri kwamba amekuwa akiumiza kichwa kuchagua nani ampange golini kati ya Aishi Manula au Beno Kakolanya.

 

Hilo limekuja ikiwa ni baada ya Kakolanya kujiunga na Simba msimu huu akitokea Yanga na kuanza kuonyesha makali yake na kumpa changamoto Manula ambapo awali aliikosa.

 

Katika mchezo wa juzi wa kirafiki dhidi ya Bandari ya Kenya uliopigwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar, kipa huyo alifanikiwa kuokoa michomo mingi ya hatari, hali iliyosababisha Mbelgiji huyo kukiri ubora wake umeleta changamoto kubwa kwa kipa wa zamani Aishi Manula.

 

Akizungumza na Championi Jumatatu, Aussems alisema kuwa kwa upande wake Tanzania ina makipa bora wawili ambao wote kwa sasa wapo ndani ya timu yake, hali inayompa ugumu kuchagua wa kikosi cha kwanza kutokana na wote kuonyesha ubora mkubwa uwanjani.

 

“Binafsi nilishasema tangu msimu uliopita kwamba Tanzania ina makipa wawili bora ambao ni Aishi na Beno, japo Beno hatukuwa naye ila sasa tupo naye na kila mmoja ameona alichokifanya kwenye mchezo wa leo (juzi), amefanya kazi kubwa ambayo kila mmoja ameipenda.

 

“Aishi yeye alikuwa benchi, lakini Beno amefanya kazi kubwa kutokana na ubora alionao, ukweli linakuwa suala gumu la kuchagua nani aanze kati yao kutokana na ubora wa viwango vyao japo Aishi ni namba moja na Beno ni namba mbili lakini wote wanafanya kazi kubwa kuanzia mazoezini,” alisema Aussems.

Dar es Salaam

Comments are closed.