The House of Favourite Newspapers

Kakunda Akabidhi Ofisi kwa Bashungwa

Wizara ya Viwanda na Biashara imesema kuwa kamwe haiwezi kushindwa katika utendaji kazi huku ikitoa mambo muhimu kwa watumishi wake wanapaswa kuyazingatia katika kutimiza azma ya Rais Dk. John Magufuli, kuifanya Tanzania kuwa nchi ya uchumi wa kati.

 

Hayo yamesemwa jana jijini Dodoma na Waziri wa Viwanda na Biashara, Innocent Bashungwa, wakati akiongea na watumishi wa wizara hiyo baada ya kukabidhiwa ofisi na aliyekuwa Waziri wa Viwanda na Biashara, Josephat Kakunda, ambaye uteuzi wake ulitenguliwa na Rais Dk. Magufuli.

 

“Siku zote siamini katika kushindwa na falsafa hiyo lazima ishuke kwa watumishi,”amesisitiza Bashungwa. Bashungwa amesema kuwa wizara hiyo ni muhimu katika kufikia azma ya kuifanya Tanzania kuwa taifa lenye uchumi wa kati ambao unatokana na maendeleo ya viwanda.

 

Aidha, Waziri Bashungwa ameyataja mambo matano ambayo ataanza kuyatilia mkazo na kuwataka wafanyakazi kushirikiana kutimiza majukumu ya kuwatumikiwa Watanzania.

 

“Kwanza lazima tutumie fursa ya miundombinu iliyopo katika kuwezesha maendeleo ya viwanda. Rais ametoa mabilioni ya fedha kujenga reli, bwawa la kuzalisha umeme, barabara, umeme na mawasiliano.

Hatua ya pili amesema kuwa ni kufanya utafiti utakaobaini mahitaji ya wakulima hususan katika kupata nyenzo za kilimo.

 

“Katika hili, TIRDO, CARMATEC na SIDO mjiandae, serikali imeweka mipango mingi ya kuongeza uzalishaji kwenye kilimo, hivyo taasisi hizo zinapaswa kuja na mkakati wa kuwawezesha wakulima kupata nyenzo za kuboresha thamani kwenye mazao,” amesema Bashungwa.

 

Ametaja hatua ya tatu ni kubainisha ni kubaini utendajikazi wa viwanda vilivyobinafsishwa na vile ambavyo havifanyikazi, hatua zipi zinapaswa kuchukuliwa kwa wakati. Bashungwa amemalizia kwa kutaja hatua ya nne ni kuwepo ushirikiano baina ya idara za masoko na biashara kwenye wizara ya viwanda na ile ya kilimo.

 

Aidha amewaomba watumishi kutekeleza mpango mkakati uliopo ili kuleta matokeo chanya kwa vitendo.

Awali, Joseph Kakunda ambaye alikuwa waziri wa wizara hiyo, amesema kuwa katika kipindi cha utumishi wake amejifunza umuhimu wa Wizara ya Viwanda na Biashara ambapo mara nyingi watu wamekuwa wakiilaumu na kuisifu.

 

Naye Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhandisi Stella Manyanya, amesema kuwa ni muhimu changamoto zilizobainika kwenye wizara hiyo zikatumika kama njia ya kuelekea kwenye mafanikio.

 

Aliwataka watumishi kufanyakazi bila kukata tama kwa kumpa ushirikiano Waziri Bashungwa ili aweze kutimiza majukumu aliyopewa.

Comments are closed.