Tanzia: Kamanda Shana Afariki Dunia
ALIYEKUWA Ofisa Mnadhimu wa Chuo cha Polisi Moshi (CCP), Jonathan Shana, amefariki dunia usiku wa kuamkia leo Jumatano, Septemba 16, 2020 katika Hospitali ya Taifa Muhimbili jijini Dar es Salaam alipokuwa akipatiwa matibabu.
Shana aliyewahi kuwa Kamanda wa Polisi mikoa mbalimbali ikiwemo Simiyu, Pwani, Mwanza na Arusha, amefikwa na mauti usiku wa kuamkia leo Jumatano tarehe 16 Septemba 2020.
Msemaji wa Hospitali ya Muhimbili, Aminiel Aligaesha, amethibitisha kutokea kwa kifo hicho cha Shana akisema amefikwa na mauti baada ya kulazwa hospitalini hapo kwa siku 21 kati ya hizo tatu alikuwa chumba cha wagonjwa wanaohitaji uangalizi wa karibu (ICU).
Mrisho Gambo, aliyekuwa mkuu wa mkoa wa Arusha wakati Shana akiwa kamanda wa polisi wa mkoa huo, ameandika katika ukurasa wake wa Instagram “Nimepokea kwa masikitiko makubwa taarifa ya kifo cha Kamanda Shana.”
“Wiki iliyopita nilikwenda kumuona Muhimbili ambako alilazwa karibuni wiki tatu na nilipata matumaini makubwa. Jamani Kamanda Shana! Bwana ametoa na ametwaa – Jina la Bwana libarikiwe,” ameandika Gambo ambaye kwa sasa ni mgombea ubunge Arusha Mjini kupitia CCM.