The House of Favourite Newspapers

Kanoute Afumua Kikosi Simba SC

0

GUMZO kubwa hivi sasa kwa mashabiki wa Simba ni kiungo mpya raia wa Mali, Sadio Kanoute ambaye upo uwezekano mkubwa wa kuwaondoa kwenye kikosi cha kwanza mastaa wawili. Hiyo ni baada ya kuonesha kiwango kikubwa katika mchezo wa kirafiki dhidi ya TP Mazembe ya DR Congo, uliochezwa juzi kwenye Uwanja wa Mkapa, Dar es Salaam.

 

Nyota huyo amejiunga na Simba hivi karibuni kwa ajili ya kuiimarisha safu ya kiungo ya timu hiyo. Kanoute huenda akahatarisha nafasi ya kucheza ya Jonas Mkude na Mzamiru Yassin katika kikosi cha kwanza cha Kocha Mfaransa, Didier Gomes.

 

Akicheza kwa mara ya kwanza kwenye Uwanja wa Mkapa, kiungo huyo alionesha kiwango kikubwa akiwa pacha na Mganda, Taddeo Lwanga.

 

Katika mchezo huo ambao Simba walifungwa bao 1-0, Kanoute alichezeshwa namba 6, huku Lwanga akicheza namba 8, wawili hao walikuwa wakibadilishana wakati mchezo huo unaendelea.

 

Kanoute alikuwa akitimiza majukumu yake yote ya uwanjani ikiwemo kunyang’anya mipira kutoka timu pinzani sambamba na kuichezesha timu yao.

 

Kiungo huyo kabla ya mchezo huo dhidi ya TP Mazembe kupigwa, alisema: “Nimekubali kusaini na kuichezea Simba kutokana na malengo ya timu ambayo yapo, kikubwa naomba sapoti kwa mashabiki wa Simba.”

 

Kutokana na kiwango chake, mtathimini viwango wa Simba SC, Mzimbabwe, Culvin Mavhunga, amefunguka kuwa: “Sadio ni mchezaji mzuri, tangu amejiunga na klabu yetu amefanikiwa kuonesha kiwango bora kwenye mechi za kirafiki ambazo tumecheza.

 

“Ni mchezaji mwenye bidii na anajituma kuanzia mazoezini. Tunatarajia makubwa kutoka kwake msimu huu kwenye ligi na michuano ya kimataifa kwa kushirikiana na wachezaji wenzake, nina imani watakuwa msaada mkubwa ndani ya kikosi chetu.”

WILBERT MOLANDI NA HUSSEIN MSOLEKA, Dar

Leave A Reply