The House of Favourite Newspapers

Kanoute, Onyango warejesha matumaini Simba SC

0

NYOTA watatu wa Simba, Joash Onyango, Sadio Kanoute na Jonas Mkude, huenda wakawa sehemu ya kikosi hicho kitakachocheza dhidi ya Dodoma Jiji, kesho Ijumaa kwenye Uwanja wa Jamhuri, Dodoma.

 

Hiyo ni baada ya kukosekana katika mchezo wa Jumanne wa Ligi Kuu Bara dhidi ya Biashara United uliopigwa kwenye Uwanja wa Karume huko mjini Musoma. Nyota hao wamekosekana kwa sababu mbalimbali ikiwemo majeraha na matatizo ya kifamilia.

 

Kwa mujibu wa mratibu wa timu hiyo, Abbas Ally, Onyango, Kanoute waliukosa mchezo dhidi ya Biashara kutokana na majeraha waliyoyapata katika mchezo wa Ngao ya Jamii dhidi ya Yanga uliochezwa Uwanja wa Mkapa, Dar.

 

Ally alisema kuwa wachezaji hao wamepona majeraha yao na huenda wakasafiri na timu kuelekea Dodoma kwa ajili ya mchezo dhidi ya Dodoma Jiji utakaopigwa Ijumaa hii kwenye Uwanja wa Jamhuri mkoani huko.

 

Aliongeza kuwa kiungo wao Mkude amemaliza matatizo ya kifamilia huku Lwanga akimalizia adhabu ya kadi nyekundu aliyoipata mchezo wa Ngao ya Jamii, hivyo atakuwa sehemu ya kikosi kitakachocheza dhidi ya Dodoma.

 

“Katika mchezo wetu huu wa kwanza wa ligi tumewakosa wachezaji wanne kwa matatizo mbalimbali ikiwemo majeraha, matatizo ya kifamilia na adhabu ya kadi.

 

“Wachezaji hao ni Onyango, Kanoute, Mkude na Lwanga ambao wote wachezaji muhimu na tegemeo katika kikosi chetu cha Simba.

 

“Wachezaji hao wakiwemo majeruhi Onyango na Kanoute wamepona, Mkude amemaliza matatizo ya kifamilia wakati Lwanga akimalizia adhabu yake ya kadi nyekundu, hivyo wataungana na timu mkoani Dodoma kwa ajili ya mchezo wa Dodoma Jiji,” alisema Ally.

WILBERT MOLANDI, Dar es Salaam

Leave A Reply