The House of Favourite Newspapers

KANSELA ANGELA MERKEL AMPIGIA SIMU RAIS MAGUFULI

Kansela wa Ujerumani Angela Merkel jana tarehe 20 Machi, 2019 amezungumza kwa njia ya simu na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli na kumhakikishia kuwa Ujerumani ipo tayari kukuza zaidi uhusiano wake na Tanzania hususani kusaidia juhudi za kuimarisha uchumi.
Angela Markel amempongeza Rais Magufuli kwa juhudi kubwa zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano katika kujenga mazingira mazuri ya uwekezaji ikiwemo kupambana na rushwa na kuimarisha miundombinu.

Kufuatia mafanikio hayo Angela Markel amesema Ujerumani itawaleta wafanyabiashara watakaowekeza katika maeneo mbalimbali ya kuimarisha uchumi ikiwemo kujenga kiwanda cha kuzalisha mbolea ambacho kitakuwa kikubwa kuliko vyote Barani Afrika.

 

Angela Merkel amesema Ujerumani imedhamiria kuunga mkono juhudi za ujenzi wa viwanda nchini Tanzania na kwamba ana matumaini kuwa kiwanda kikubwa cha mbolea kitakachojengwa nchini Tanzania kitasaidia kuongeza kipato cha wananchi na kuimarisha kilimo kwa Tanzania na nchi nyingine za Afrika.

 

Ametoa wito wa kuimarishwa kwa Tume ya Kudumu ya Pamoja ya Ushirikiano (Joint Permanent Comission – JPC) na amemwalika kwa mara ya pili Rais Magufuli kutembelea Ujerumani, ziara ambayo itatanguliwa na ziara ya Mawaziri wa Tanzania kukutana na Mawaziri wa Ujerumani.

 

Kwa upande wake Rais Magufuli amemshukuru Angela Merkel kwa kumpigia simu na kueleza dhamira yake ya kukuza zaidi uhusiano wa Tanzania na Ujerumani na amebainisha kuwa Tanzania itahakikisha inajenga mazingira mazuri katika maeneo yote ya ushirikiano yakiwemo biashara na uwekezaji.

 

Rais Magufuli amempongeza Mhe. Angela Markel kwa uongozi wake wa zaidi ya miaka 13 akiwa Kansela wa Ujerumani na amemhakikishia kuwa Tanzania itadumisha na kukuza zaidi ushirikiano huo kwa manufaa ya pande zote mbili.

Comments are closed.