The House of Favourite Newspapers

KASI YA SIBOMANA YAMKOSHA ZAHERA

KASI ya winga wa Yanga, Patrick Sibomana raia wa Rwanda ya kushuka na kupandisha mashambulizi imemkosha kocha mkuu wa timu hiyo, Mwinyi Zahera na kuweka wazi kwamba alikuwa anamuhitaji mtu wa namna hiyo ndani ya timu hiyo ili aweze kufanya vizuri na kutwaa mataji.

 

Zahera amesema hayo ikiwa ni baada ya Sibomana kusajiliwa katika dirisha la msimu huu akitokea Mukura Victory ya kwao Rwanda. Nyota huyo hadi sasa amefanya makubwa katika klabu hiyo ikiwa ni pamoja na kufunga mabao saba katika mechi nane za kirafiki walizocheza timu hiyo.

 

Akizungumza na Spoti Xtra, Zahera amesema kuwa kasi ya winga huyo sambamba na wachezaji wengine ambao wamesajiliwa kwa sasa akiwemo Juma Balinya inampa matumaini ya kufanya vizuri kutokana na kutibu tatizo ambalo alikuwa nalo msimu uliopita.

 

“Timu ya msimu uliopita ina tofauti sana na hii ambayo ninayo kwa sasa. Msimu uliopita ilikuwa kwamba kama ikitokea timu inapoteza mpira basi inakuwa shida kwa sababu wachezaji wanatembea tu.

 

“Lakini kwa wachezaji wapya hawa utaona kama wanashambulia basi wanapanda wengi lakini kama tunapoteza mpira basi wanakimbia haraka kuja kukaba. Kwa aina ya watu hawa ambao nilikuwa ninawataka nina uhakika mkubwa kwamba tutafanya vizuri kwenye msimu huu,” alisema Zahera

Comments are closed.