IKIWA ni muda mfupi baada ya Rais John Magufuli kusema kuwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola na baadhi ya wasaidizi wake wamefanya mambo ya hovyo hivyo hawatakiwi kuendelea kuwepo kwenye wizara hiyo, waziri huyo amezungumza kuhusu uamuzi huo wa rais.
“Rais ndiye aliniteua kwenye baraza la mawaziri na ndiye ameona anipumzishe, kwangu mimi ni jambo la faraja. Watanzania mmemsikia Rais hatua aliyochukua ni hatua nzuri na inalenga kujenga safu ya serikali, ninaahidi kama mbunge ambaye nilipata nafasi ya kumsaidia rais nitaendelea kumsadia kwa kwa heshima kubwa.
“Narudia kama kuna wizara inanitesa ni ya Mambo ya Ndani, inatesa sana, kuna tume nyingi sana zimeundwa kuchunguza wizara hii kwa miradi ya hovyo iliyokuwa ikifanyika na nilitegemea watu watajifunza, kuna mradi wa ajabu umetengenezwa kwenye wizara hii wa Euro milioni 408.
“Mradi huu wa Euro milioni 408 umetayarishwa na kusainiwa na Kamishna Jenerali wa Fire, haujapangwa kwenye bajeti, haujapitishwa na bunge, wakati wa vikao vya majadiliano Romania wahusika wote wa Tanzania wanalipwa ‘Sitting Allowance’ ya Dola 800 bado tiketi za ndege.
“Nampongeza sana Meja Jenerali Kingu aliyekuwa Katibu Mkuu wa Mambo ya Ndani kwa kuamua kuwajibika na kujiuzulu na nitaendelea kumheshimu kwa hili, lakini Lugola na wengine narudia hapana, kwenye ‘position’ hii NO!
“Kwenye hili sakata kuna hadi Ofisi ya Mwanasheria Mkuu, kuna watu walisubiri Mwanasheria Mkuu amefiwa na mke wake wakaenda kupitisha, wakaandika na kwa niaba, najua mnamhurumia Lugola lakini acha akajifunze.
“Nasema tena Kangi Lugola nampenda sana, ni mwanafunzi wangu pamoja na mwili wake na ukubwa wake ni mwanafunzi wangu nimemfundisha Sengerema Sekondari lakini kwa hili hapana. Kamishna Jenerali Andengenye kwa hili pia hapana, kwa utawala wangu hapana. Ni mara kumi nisiwe rais nikakae kwetu Chato lakini kwa wakati huu nikiwa rais lazima niwaambie ukweli, lazima mambo yaende bila ujanjaujanja.