The House of Favourite Newspapers

Kauli ya Kwanza ya Rais Karia wa TFF Baada ya Kuapishwa

0
Wallace Karia akiapishwa kuwa Rais wa TFF.

KUFUATIA Uchaguzi Mkuu wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) uliofanyika leo katika Ukumbi wa St Gasper Mjini Dodoma na kumalizika jioni ya leo, Mwenyekiti wa Kamati ya TFF, wakili Revocatus Kuuli ametangaza matokeo ya Uchaguzi huo Wallace Karia ameshinda nafasi hiyo kwa jumla ya kura 95 kati ya kura halali 125 zilizopigwa huku kura tatu zikiharibika na Michael Wambura akichaguliwa kuwa Makamu wa Rais wa Shirikisho hilo..

 

Wagombea wengine wa Urais pamoja na kura walizopata ni Ally Mayay Tembele (9), Shija Richard (9), Iman Madega (8), Frederick Mwakalebela (3) na Emmanuel Kimbe (1).

Karia akizungumza baada ya kuapishwa.

 

Wajumbe wa Kamati ya Utendaji walioshinda kwenye uchaguzi wa leo pamoja na Kanda wanazoziwakilisha kwenye mabano ni kama ifuatavyo:

Mohamed Abeid (Dodoma na Singida), Mbasha Matutu (Shinyanga na Simiyu), Sarah Chao (Arusha na Manyara), Dustan Ditopile (Lindi na Mtwara), Elias Mwanjala (Mbeya na Iringa), Francis (Pwani na Morogoro), Vedastus Lufano (Mara na Mwanza), Lameck Nyangaya (Dar es salaam), Kenneth Pesambili (Rukwa na Katavi), Khalid Mohamed (Kilimanjaro na Tanga), Issa Mrisho (Kigoma na Tabora) na James Patrick (Njombe).

Rais wa Shirikisho hilo, Wallace Karia, Makamu wa Rais, Michael Richard Wambura pamoja na Wajumbe wa Kamati ya Utendaji waliochaguliwa wameapishwa leo mjini Dodoma muda mfupi baada ya matokeo ya ushindi wao katika uchaguzi huo kutangazwa.

 

Richard Wambura akiapishwa kuwa Makamu wa Rais wa TFF.

Akitoa hotuba yake muda mfupi baada ya kuapishwa kwake, Rais wa Shirikisho hilo (Wallace Karia) amesema kuwa amepigiwa simu na Rais wa Shirikisho la Soka Duniani (FIFA), Gianni Infantino pamoja na Rais wa Shirikisho la Soka Afrika (CAF), Ahmad Ahmad na wote wamelipongeza Shirikisho hilo kwa uamuzi ulioufanya na kuutakia uongozi mpya mafanikio mema.

Aidha Karia amesema TFF itawapa waandishi wa habari elimu ili kujua mambo gani ya kuzingatia kuweza kuinua soka la Tanzania, huku akitangaza kuanzia leo, soka la Tanzania halitakuwa na ubabaishaji.

Kwa upande wake, Waziri mwenye dhamana ya Michezo, Dkt. Harrison Mwakyembe ameiagiza TFF kuweka utaratibu wa kuchapisha taarifa ya mapato na matumizi kwenye magazeti ili wananchi wajue.

Musa Mateja | Global Publishers | Dodoma

VIDEO YA MATOKEO HAYO

Leave A Reply