KCB Yaingia Mkataba wa Mil. 500 na TFF
BENKI ya KCB leo Septemba 13, 2020 imesaini mkataba na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kwa ajili ya kudhamini Ligi Kuu Bara kwa msimu wa 2020/21.
Mkuu wa Idara ya Masoko wa KCB, Christine Manyenye, amesema:”Tuna furaha kubwa kwa kudhamini shilingi milioni 500 na kodi ndani yake licha ya ugumu ambao upo kwa sasa kutokana na uwepo wa janga la Corona ambalo limeisumbua dunia na kwa sasa bado lipo.
“Malengo yetu ni kuona kwamba kunakuwa na ushindani ndani ya ligi pamoja na kuona kwamba kila mwanafamilia wa michezo anafurahi na ajira inapatikana kupitia michezo.
“Pia KCB lengo letu ni kuona kwamba tunaweza kuwa sehemu ya mafanikio ya wengine pamoja na kukuza uchumi wa nchi kwa kuwa michezo ni ajira na tunalipa kodi,” alisema.
Mwenyekiti wa Bodi ya Ligi, Steven Mguto, kwa niaba ya Rais wa TFF, Wallace Karia, amesema kuwa sapoti inaayotolewa na KCB ni kubwa na kufanya hivyo ni kurudisha fadhila kwa jamii na ni sehemu ambayo imekuwa na mwitikio mkubwa.
“Tunaingia mwaka wa nne tukiwa na KCB, tuna uhakika kwamba hiki wanachokitoa ni kikubwa kwa ajili ya masuala ya michezo,” alisema.