The House of Favourite Newspapers

Rais wa TLS, Mwabukusi Aipinga Tafsiri ya NEC Kuhusu Maadili ya Uchaguzi

Rais wa Chama cha Wanasheria wa Tanganyika TLS, Wakili Boniface Mwabukusi

Rais wa Chama cha Wanasheria wa Tanganyika TLS, Wakili Boniface Mwabukusi ameeleza kusikitishwa na tafsiri ya sheria inayochukuliwa na Tume huru ya Taifa ya uchaguzi, akisema hakuna sheria inayozuia Chama cha siasa kushiriki uchaguzi kwa kutosaini Kanuni za maadili ya uchaguzi.

Kupitia ukurasa wake wa X Mwabukusi ameandika kusema;

“Sijui hawa wenzetu wanazisomaje hizi sheria, Je ni utofauti wa vyuo? Hakuna sheria inayozuia chama kushiriki uchaguzi kwa kutosaini maadili ya uchaguzi ni tafsiri mbovu ya kukosa logic (maana). Tuache kuharibu Taifa na kuchochea vurugu.” ameandika Wakili Mwabukusi.

Jana Aprili 12, Vyama 18 vyenye usajili wa kudumu nchini Tanzania vilisaini kanuni za maadili ya uchaguzi mkuu wa Mwezi Oktoba mwaka huu na kulingana na Mkurugenzi wa Uchaguzi Ramadhan Kailima, @ChademaTz haikufika kusaini kanuni hizo suala ambalo limeelezwa kuwa kutokana na kutosaini kwao wamepoteza sifa ya kushiriki uchaguzi mkuu na chaguzi ndogo zitakazofanyika ndani ya miaka mitano 2025/30.