The House of Favourite Newspapers

Kessy Amtumia Salamu Okwi, Kichuya

Hassan Kessy mwenye jezi namba 22

BEKI Mtanzania anayeichezea Nkana FC ya Zambia, Hassan Kessy, amesema hana hofu kabisa mara watakapokutana na Simba kutokana na kuzijua mbinu zao huku akiwatumia salamu viungo washambuliaji Mganda, Emmanuel Okwi na Shiza Kichuya.

 

Kauli hiyo aliitoa saa chache mara baada ya kufanikiwa kuwaondoa wapinzani wao UD Songo kutoka Msumbiji kwa ushindi wa jumla ya mabao 3-1 katika hatua ya awali ya Ligi ya Mabingwa Afrika.

 

Timu hizo zinatarajiwa kuvaana Desemba 14, mwaka huu mchezo utakaopigwa nchini Zambia, kabla ya kurudiana kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, Desemba 21, mwaka huu.

Wachezaji wa Simba kutoka kushoto ni Emmanuel Okwi, Chama (katikati) na anayekuja ni Kagere.

Akizungumza na Championi Ijumaa kutoka Zambia, Kessy alisema hakuna mchezaji asiyemjua kwenye kikosi cha Simba, huku akiwa na matarajio makubwa ya kuwaondoa katika hatua inayofuata ya michuano hiyo.

 

Alieleza kuwa, anafurahia kukutana na wachezaji anaojua aina yao ya uchezaji wao, hivyo hatakuwa na kazi kigumu na badala yake atajipanga yeye pamoja na wenzake ili kuhakikisha wanafakisha malengo yao ya kufika mbali kimataifa.

 

“Nusu ya wachezaji waliokuwepo Simba wote nimecheza nao, ni wachache

ambao sijacheza nao lakini wengi wao wananifahamu na mimi ninawafahamu vizuri wakiwemo hao akina Okwi na Kichuya nitakaokutana nao katika nafasi yangu ninayocheza.

“Binafsi nitatimiza majukumu yangu ya ndani ya uwanja nitakayokuwa nayo kuzuia na kupunguza mashambulizi ambalo ndilo jambo la msingi,” alisema Kessy.

Comments are closed.