The House of Favourite Newspapers

Kiba, Namba Hazidanganyi Mzee Baba

Ali Saleh Kiba

ALI Saleh Kiba ndiyo ma­jina matatu yanayo­tambulika kiseri­kali. Mengine ni King Kiba au Ali Kiba. Mzee Baba ni swaga tu ya kumpamba mtu inayo­tumiwa na watoto wa mjini kuonesha kuwa unakubalika.

 

Kiba wewe ni bonge moja la mwanamuziki wa Bongo Fleva na Afro-Pop kwa jumla. Najua mbali na uimbaji pia wewe ni mtunzi mzuri wa nyimbo kali chini ya Lebo ya Rockstar4000 ambayo wewe ni mkurugenzi wake. Hongera! Sina shaka na kipaji chako chenye tofauti na wanamuziki wenzako. Unaweza kuwa miongoni mwa wa­namuziki watano bora kabisa kuwahi kutokea kwenye Bongo Fleva.

 

Tunajua na wewe mwenyewe unakumbuka mwaka 2011 ulichaguliwa kuwa Msanii Bora wa Kwanza wa Afrika Mashariki ukiwakilisha Tanzania, Kenya na Uganda. Mwaka 2015 ulishinda Tuzo Tano za Kili na kuthibiti­sha kuwa wewe ni bora ukilin­ganisha na mshindani wako, Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’. Itoshe tu kusema kuwa, Kiba Mzee Baba dunia inakujua na inajua muz­iki wako.

 

Ushindani wako na Diamond ume­sababisha muziki huu kufika mbali zaidi. Bila ninyi, pen­gine leo tungekuwa tunazungumza anguko la muziki huu kama ilivyo kwa muziki wa dansi. Kwa bahati nzuri mmetengeneza aina ya ushindani unaoelekea kuwa kama uadui lakini ndani yake kuna biashara kubwa. Ni ushindani wa nani zaidi kati yenu! Ni ushindani ambao unahitajika kwenye muziki ili kuleta chachu kiroho safi.

Mara ya mwisho kwa wasanii wa Tanzania kuwa na ushindani wa namna hii ilikuwa yapata miaka saba iliyopita. Kulikuwa na waigi­zaji wawili maarufu wa filamu hapa Tanzania, Vincent Kigosi ‘Ray’ na marehemu Steven Kanumba.

 

Ray na Kanumba walikuwa walikuwa na upinzani mkali katika wakati ambao ninaweza kusema ulikuwa wa dhahabu katika tasnia ya filamu hapa nchini. Kila baada ya miezi mitatu kulikuwa na filamu mpya kutoka kwa mmoja wao.

 

Kukaibuka vibanda vingi vya kuu­za filamu za Kibongo. Wakati wote huo, Ray na Kanumba walikuwa wakiishi kama maadui. Huyu ak­isema hili, huyu anasema lile.Tofauti ya ushindani wa Ray na Kanumba na huu wa Kiba na Diamond ni mitandao ya kijamii pekee, lakini upinzani huu yafaa kuwa wa jadi kwani unatia chachu kwa mashabiki wenu.

 

Baada ya hapo tujadili kidogo kili­chojiri mara tu ulipoachia ngoma yako mpya ya Mvumo wa Radi na ikawa kama imesimama kiasi fulani ilipofiki­sha views laki saba na themanini, kabla ya kuiruhusu na sasa inakimbilia views milioni mbili. Kiba nilikusikiliza kwa umakini mkubwa ulipodai kuwa, kuna mchezo mchafu wa wasanii kununua views (watazamaji wa ngoma) katika Mtandao wa YouTube.

 

 

Kama utakumbuka, wakati una­toa kauli ile, ilikuwa ni siku moja tu imepita tangu ngoma yako hiyo iingie YouTube na kupata tatizo. Tatizo lenyewe ilikuwa ni kwamba idadi ya views ilisima­ma na baadaye kushuka kabisa hivyo kuibua sintofahamu.

 

Mzee baba ulionekana kama kupaniki fulani hivi. Ulisikika ukisema kwamba suala la ununuzi wa views lipo, tena sana ila kwako halina maana.Ulikiri kwamba, kuna suala la kuweka maro­boti kwenye YouTube ambao kazi yao ni kuongeza views. Ulimalizia kwa kusema kuwa, wewe hufanyi jambo kama hilo na kwamba kufanya hivyo ni utoto badala yake wewe unafanya muziki kwa ajili ya watu hivyo huwezi kuwadanganya.

 

Pia ulidai kwamba, pamoja na tatizo hilo la kusimama kwa views na baadaye kushushwa hakukuathiri muziki wako.Katika ufafanuzi wa YouTube ni kwamba walibaini uwepo wa maroboti wa kununuliwa kwa ajili ya kuongeza views wapatao elfu the­lathini hivyo kuwaondoa na kubaki laki saba na nusu!

 

Tafsiri ni hii, kinachoonekana Kiba ndiye aliyedaiwa kununua views ndiyo maana Youtube wakaishikilia akaunti yake, wakati views wakiwa laki saba na themanini. Walipoi­fanyia ukaguzi iligundulika kuwa kulikuwa na maroboti elfu thelathini hivyo walipowaondoa akabakiwa na views laki saba na hamsini ndipo wakaiachia video hiyo.

 

Kiukweli Kiba hapo ulipaswa kukubali kuwa namba hazidanganyi kuliko kuendelea kung’ang’ania tu kuwa kuna wasanii wananunua views bila kuwataja huku mwenyewe ukiwa umekamat­wa na maroboti elfu thelathini! Hata hivyo, tunajua kuwa hata ukinunua views huwezi kukiri.

 

Ukweli Kiba ni kwamba namba hazidanganyi labda utoe ushahidi wa wasanii wanaonunua views. Lakini hadi sasa ushahidi unaonesha wewe ndiye unadaiwa kununua views na ndiyo maana YouTube walishikilia akaunti yako na kuondoa views feki za maroboti.

Kwa hiyo mimi naona wewe siyo mtu sahihi wa kukemea jambo hilo ilihali na wewe ni mtuhumiwa wa kununua views.

Comments are closed.