Kigogo Ajiondoa Yanga; ‘Nimeamua Kujiuzulu’
ALIYEKUWA Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Yanga, Shija Richard, amejiuzulu nafasi hiyo leo Ijumaa huku akishindwa kuweka wazi sababu za kujiuzulu kwake.
Richard ni miongoni mwa wajumbe watatu wanaotuhumiwa kutokuwa na mahusiano mazuri na Kampuni ya GSM ambayo hivi karibuni ilitangaza kubakia kuwa mdhamini kama mkataba wake unavyoelekeza. Wengine wanaotuhumiwa ni Rodgers Gumbo na Salim Rupia.
Katika taarifa yake aliyoitoa leo, Richard amedai kuwa klabu hiyo ni kubwa kuliko mtu hivyo ameamua kujiweka pembeni.
“Nimeamua kwa hiari yangu kujiuzulu nafasi zote za uongozi katika klabu yangu ya Yanga.
“Yanga ni kubwa kuliko mimi na kuliko mtu yeyote. Yamezungumzwa mengi lakini mimi sitazungumza chochote. Wakati utaongea.
“Ukweli hata usipousema, huwa una tabia ya kujitokeza wenyewe japo taratibu, lakini huwa unadumu milele. YANGA DAIMA MBELE NYUMA MWIKO”, imefafanua barua hiyo.