The House of Favourite Newspapers

KIJIKO CHA JIKONI, HAKIOGOPI MOTO !

SHUUUUTUUUU! Jitu zima hovyo kutwa kuwasema wamama wenzio, hivi jamani mtu kufanikiwa kidogo ndo yamekuwa maneno? Basi yachukue kayachapishe kwenye kanga uvae! Heee heeeiyaaa na mwaka huu mtanuna sana, kutwa kuogea sabuni za miche, hebu mtupishe siye waogea sabuni za Kizungu!  Shoga leo nimekereka hadi nimesahau kuwasalimu, itikia basi na wewe siyo umevimbisha mijicho kama umepewa taarifa mumeo anachepuka na jirani yako! Haloooo eeeehhh tena ya kisoda ya bia nitalewa miye, nashanga’ shoga, tangu lini maji ya dafu yakapikia chai!

Baada ya udambwidambwi shoga leo nipo na nyie kina baba ambao mkimuona kidogo mkeo anachati basi akili zenu moja kwa moja mnazielekezea kwa michepuko! Mtu asichati na ndugu yake, asichati na mama yake?

Bora basi umbane mkeo kuangalia simu yake, yako kutwa umejaza minamba ya

siri hadi mwenyewe ukitaka kuitoa lazima ufikirie mara mbilimbili, kwa taarifa yako mwanamke wa baa hatongozwi asubuhi! Kama mkeo akiamua kukudanganya kwenye simu anaweza sana kwa hiyo we jishaue tu kumbana kama unakamata njiwa bandani!

Kuna wakati nikisikia mwanamke mwenzangu ananyanyasika kwa sababu ndogo shoga huwa inaniuma, sawa wanawake sisi wakati mwingine tunaweza kusema akili zinafanana, na nyie je? Maisha siku hizi yamebadilika ati! Kama ulidhani kuweka minamba ya siri kwenye simu yako unamkomoa mkeo unajidanganya! Mlevi hachagui pombe, weeeeeraaaaaa!

Shoga kama kweli alikuoa kwa shida na raha, kwa namna yoyote ile basi jiwekeeni maisha yenu huru, akitaka simu mpe na yeye ukitaka yake akupe, hayo manamba ya siri ya kizamani tena inaleta picha kuwa hamuaminiani, upo nyonyo?

Wanaume wengine ndiyo imeshakuwa sehemu ya kutafuta sababu za kukuacha, ukiona anakuandama hivi jua ana kimada wake anatafuta upenyo wa kuishi naye! Ngoja nikung’ate tu sikio shoga yangu, kijiko cha jikoni hakiogopi moto! Kama kweli anakupenda na umemzalia watoto, anakimbilia simu yako atafute nini? Akikutana na meseji za bahati mbaya atakuelewa huyo?

Tusikaushane uzazi, janaume wewe badilika, kuwa muelewa, kama kweli umedhamiria kuangalia simu ya mkeo basi na wewe uwe huru kwenye simu yako na kama haujadhamiria kuangalia basi muishi bila wasiwasi! Kwa leo naomba niishie hapa, ni mimi Anti Naa Shangingi Mstaafu!

Comments are closed.